Jul 25, 2013

HIKI NDICHO ALICHOKISEMA MNYIKA BAADA YA CHENGE KUSEMA KODI YA (SimCardTax) NI SAHIHI

Chenge (Mb) amesema kodi ya kadi za simu (SimCardTax) ni sahihi kwa utafiti wao; aulizwe kupitia 0754782577 atoe maelezo zaidi na vielelezo vya ziada

Leo tarehe 25 Julai 2013 chombo kimoja cha habari kimemnukuu Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti Andrew Chenge (Mb) akisema kwamba uamuzi kuhusu kodi/tozo ya kadi/laini za simu haukuwa wa kubahatisha. Chenge amesema kwamba kamati yake ilifanya utafiti wa kina na kisha kufikia uamuzi wa kuona tozo hiyo ni sahihi.

Ni muhimu akatakiwa kupitia namba yake 0754782577 atoe maelezo zaidi kuhusu usahihi wa tozo hiyo na aeleze ni wapi wananchi na wadau mbalimbali wanaweza kupata vielelezo vya utafiti walioufanya.

Aidha, wenye maswali kuhusu nini hasa kilijiri kwenye kamati ya bajeti mpaka kamati hiyo ikakataa jedwali la marekebisho nililowasilisha tarehe 27 Juni 2013 kabla ya muswada wa sheria ya fedha kupitishwa bungeni tareheb 28 Juni 2013 kwa kuwa yeye ambaye ndiye msemaji wa kamati ameanza kutoa majibu.

Pia, aeleze iwapo yupo tayari kumshauri Spika aruhusu kamati ya bajeti ikutane kwa dharura wiki ijayo kufanya kazi ya kupitia matumizi ya Serikali kwa lengo la kuanisha maeneo ambayo Serikali inaweza kubana matumizi kwa haraka kufidia pengo la bilioni 178 zinazotafutwa kwenye tozo hiyo ya simu. Hatua hii itawezesha kodi hiyo kuacha kutozwa bila ya kulazimika hata kuongeza vyanzo vingine vya fedha iwapo Serikali inasuasua kupanua wigo wa mapato.

Izingatiwe kuwa katika kuwawakilisha wananchi kuepusha kutozwa kodi ya kumiliki kadi ya simu na nyingine zenye kuongeza gharama za maisha kwa wananchi, kabla ya kupitishwa kwa muswada wa sheria ya fedha nilichukua hatua kuanzia bungeni katika mkutano uliopita wa Bunge.

Niliwasilisha kwa Bunge kupitia ofisi ya Katibu wa Bunge jedwali la marekebisho ya sheria hiyo kwa mujibu wa Kanuni ya 86 (11) ambapo pamoja na mapendekezo mengine nilitaka kifungu katika jedwali la marekebisho la Serikali kilichopendekeza kuanzisha ushuru huo kiondolewe.

Ikumbukwe kwamba kwamba katika mchango wangu kwa kuzungumza bungeni nilisema muswada wa sheria ya fedha wa mwaka 2013 ni “muswada wa majanga” ambao utaleta athari za ongezeko la bei ya bidhaa na huduma muhimu.

Hata hivyo, Kamati ya Bajeti chini ilikataa mapendekezo hayo, hata hivyo kwa kuwa masharti ya kanuni za kudumu za Bunge yanakataza mbunge mwingine kutoa taarifa za majadiliano ya ndani ya kamati sitaeleza kwa undani yaliyojiri katika kikao cha kamati tajwa.

Hivyo taarifa rasmi na sababu za mapendekezo hayo kukataliwa zinaweza kutolewa na mwenyekiti wa kamati hiyo Mh. Andrew Chenge (Mb) kwa kuulizwa kupitia namba yake ya simu ya mkononi/kiganjani (0754782577).

Uongozi bora na uraia mwema wenye uwajibikaji ni chimbuko na chachu ya ukuaji endelevu wa uchumi wa nchi na ustawi wa maisha ya wananchi.

Kwa ufupi nilielelezwa kwamba tayari chanzo hicho cha mapato na vingine vilishaingizwa katika bajeti ya Serikali kwa ajili ya matumizi ya kawaida na ya miradi ya maendeleo kwa mwaka wa fedha 2013/2014 na kupigiwa kura ya ndio na wabunge wengi kabla ya muswada huo wa sheria ya fedha kujadiliwa. Hivyo nilitakiwa kuwasilisha mapendekezo ya vyanzo mbadala vya kuziba pengo litakalotokana na kufuta ushuru huo na kodi zingine nilizopendekeza zifutwe au zipunguzwe.

Katika muktadha huo kwa upande wa sekta ya mawasiliano pekee, nilipendekeza vyanzo mbadala vyenye jumla ya zaidi ya bilioni 400 za kitanzania ambazo ni zaidi ya lengo lililowekwa na Serikali bila ya kuongeza mzigo wa gharama kwa wananchi wa kawaida. Nilitoa ushuhuda wa kitakwimu kutoka nchi ya Ghana ambayo makampuni ya simu yanachangia asilimia 10 ya mapato ya nchi hiyo bila kuongeza mzigo mkubwa wa gharama kwa watumiaji wa kawaida wa huduma za simu ya kiganjani/mkononi.

Kati ya mapendekezo niliyotoa ni pamoja na kutaka marekebisho ya Sheria ya Mawasiliano ya njia Kieletroniki na Posta ya mwaka 2009 ili kuipa uwezo wa kutosha Mamlaka ya Udhibiti wa Mawasiliano Tanzania (TCRA) kufanya ukaguzi wa uwekezaji unaofanywa na makampuni ya simu. Hata hivyo, mapendekezo hayo yalikataliwa na kamati ya fedha chini ya uenyekiti wa Andrew Chenge (Mb).

Ifahamike kuwa kwa kurejea masharti ya Kanuni ya 109 (2) niliwasilisha pia katika ofisi kwa Katibu wa Bunge kabla mjadala kuhusu muswada huo kufungwa mapendekezo ya ziada ya vyanzo mbadala vya mapato vya kuziba pengo lililotokana na marekebisho niliyotaka yafanyike kwa lengo la kupunguza mzigo wa gharama za maisha kwa wananchi kutokana na ongezeko la kodi.

Marekebisho hayo yangechangia katika kudhibiti udanganyifu unaofanywa na makampuni mengi ya simu juu ya uwekezaji na faida wanayoipata. Marekebisho hayo yangewezesha pamoja na mambo mengine makampuni mengi kuorodheshwa katika soko la hisa la Dar Es Salaam na pia kudhibiti usajili wa makampuni katika nchi zenye mfumo wa kuwezesha ukwepaji kodi (Tax Heavens).

John Mnyika (Mb)
25 Julai 2013

0 Weka maoni yako hapa:

Post a Comment

COMMENT HAPA