Aug 19, 2013

HILI NDIO TAMKO LA WAISLAM MWEMBE YANGA

Leo Waislamu walikusanyika kwa wingi katika viwanja vya Mwembe Yanga, Temeke Jijini Dar es Salaam kuwasikiliza masheikh wanatoa tamko gani kuhusu kadhia ya kujeruhiwa Katibu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Tanzania, Sheikh Ponda Issa Ponda.

Uwanja ulikuwa umefurika waumini waliokuwa na hamu kubwa ya kusikiliza kile kitakachosemwa na viongozi wao.

Tulibahatika kuhudhuria kuanzia mwanzo wa shughuli mpaka mwisho, ingawa hatukuweza kuwaletea yaliyokuwa yakiendelea moja kwa moja kutoka uwanjani kutokana na sababu zilizokuwa nje ya uwezo wetu.

Hata hivyo, muda si mrefu shughuli imekamilika. Mwitikio ulikuwa mkubwa na watu walikuwa wengi sana, uwanja wa Mwembe Yanga ulifurika hasa.

Sheikh kutoka Morogoro, aliwaelezea tukio zima la kupigwa risasi kwa Sheikh Ponda, jinsi alivyowatoroka Polisi na kile kilichofanywa na jeshi hilo katika uficha ukweli.

Baada ya Sheikh kutoka Morogoro, ilifuatia salamu ya Sheikh kutoka Zanzibar ambaye alielezea kadhia nzima ya safari ya Sheikh Ponda visiwani Zanzibar na yale aliyoyatamka dhidi ya dhulma iliyofanywa na serikali ya visiwa hivyo kwa masheikh mbalimbali. Mpaka sasa kadhaa wapo ndani na huu ni mwezi wa 10 hawajapewa dhamana. Aliwaeleza Waislamu kuwa tayari wana muungano wao, ambao ni Muuungano wa Uislamu, na hivyo hawahitaji muungano ulioasisiwa na Mzee Nyerere na Mzee Karume.

Aidha, alisema kuwa muungano wa Uislamu ni imara zaidi kuliko muungano huu unaolazimishwa na watawala.

Pamoja na mambo mengine alizungumzia tukio la kumwagiwa tindikali kwa wasichana wawili, raia wa Uingereza. Alieleza kuwa, kwa mujibu wa gazeti la Telegraph la Uingereza, matukio hayo yameongezeka huko nchini Uingereza, na hivyo kuna uwezekano kuwa wahusika wa tukio hilo wanatoka huko huko Uingereza.

Baadaya swala ya Alasiri, ilitolewa mada kuhusu harakati za Sheikh Ponda, msingi na malengo yake, pamoja na kile kilichompata Sheikh huyo.

Waislamu walikuwa na msisimko na hamasa ya ajabu mno ambayo muda mwingi watoa mada walilazimika kukatisha mada zao ili kupisha sauti za Takbirah zilizokuwa zikihanikiza uwanjani hapo.

Baada ya mada hiyo, uliwadia wakati wa tamko lililotolewa na Amiri wa Wahadhiri Tanzania, Sheikh Kondo BUngo. Yafuatayo yalikuwa katika tamko hilo la Mwembe Yanga:

1- Waislamu wanatambua kuwa Sheikh Ponda alipigwa risasi na Polisi kwa lengo la kumuua.

2- Waislamu wanataka Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro awajibishwe, ikiwa ni pamoja na kupelekwa mahakamani. Hasa ikizingatiwa kuwa wakati akiongea na vyombo vya habari vya ndani, alikanusha tuhuma za polisi kutekeleza kitendo hicho, lakini alipoongea na vyombo vya habari vya nje alikiri kuwa polisi walimpiga risasi Sheikh Ponda, kama ilivyonukuliwa na vyombo hivyo.

3- Kamanda wa operesheni ya kumkamata na kumjeruhi Sheikh Ponda, pamoja na askari aliyepigwa risasi wanatakiwa kuwajibishwa na kushitakiwa.

4- Waziri wa Mambo ya Ndani, Dk. Emmanuel Nchimbi ajiuzulu.

5- Waislamu hawaitaki tume ya polisi, bali wanataka tume huru itakayochunguza tukio hilo, kwa sababu Polisi ni waongo, na Waislamu hawana imani nao tena. Aidha, Polisi ni watuhumiwa, hivyo hawawezi kujichunguza kisha wakatenda haki.

6- Waislamu wanatangaza kuwa adui yao mkubwa kwa sasa ni serikali ya CCM, na hivyo wanakusudia kuitia adabu. Kampeni za kuitia adabu zinaanza sasa hivi mpaka mwaka 2015 wakati wa uchaguzi mkuu.

Iwapo hayo hayatatekelezwa, Waislamu wametangaza kuchukua hatua stahiki itakayoifanya iwe mwisho wa kudhulumiwa katika nchi hii.

Ndugu wadau, kwa mukhtasari hayo ndiyo yaliyojiri katika Viwanja vya Mwembe Yanga, ambapo sisi wenyewe tulikuwa mashuhuda.

HUU NI UMATI ULIOJITOKEZA JANA 

chanzo na page ya islamic forum

https://www.facebook.com/IslamicForumOfTanzania

0 Weka maoni yako hapa:

Post a Comment

COMMENT HAPA