Jun 18, 2012

Michuano Ya KAGAME Kuanza Julai 14

Mashindano ya Klabu bingwa Afrika Mashariki na Kati (Kombe la Kagame) yanayoandaliwa na Baraza la Vyama ya Mpira wa Miguu Afrika Mashariki na Kati (CECAFA) yatafanyika jijini Dar es Salaam kuanzia Julai 14-29 mwaka huu ambapo timu zinatakiwa kuthibitisha ushiriki wao kabla ya Juni 25 mwaka huu.

Yanga itashiriki mashindano hayo ikiwa bingwa mtetezi, wakati Tanzania Bara itawakilishwa na mabingwa wake Simba na Makamu bingwa Azam. Mashindano hayo yatafanyika jijini Dar es Salaam kwenye Uwanja wa Taifa na Uwanja wa Chamazi pekee kwa sababu ya kupunguza gharama za uendeshaji.

Ratiba ya mashindano hayo yanayoshirikisha mabingwa kutoka nchi kumi na moja ambao ni wanachama wa CECAFA itapangwa Juni 29 mwaka huu.

Mashindano haya ni muhimu kwa CECAFA na Tanzania Bara ambayo ndiyo mwenyeji kwa maendeleo ya mpira wa miguu na pia kukuza kiwango cha mchezo huo kwa ukanda huu ambao kwa Afrika unaoongoza kwa kufanya mashindano mengi ya timu za Taifa pamoja na klabu.

Mwenyekiti wa CECAFA ambaye pia ni Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Leodegar Tenga amewaomba wadau kujitokeza kudhamini michuano hiyo ambayo itaoneshwa na kituo cha televisheni cha SuperSport. Pia amewataka washabiki kujitokeza kwa wingi viwanjani kuunga mkono michuano hiyo.

CECAFA inawashukuru wadau wote kwa kuwezesha michuano hiyo kufanikiwa akiwemo Rais wa Rwanda, Paul Kagame kwa kutoa zawadi za fedha kwa washindi, Serikali ya Tanzania kwa kutoa Uwanja wa Taifa na Kamati ya Utendaji ya TFF kwa kukubali kuwa mwenyeji wa mashindano hayo.

Boniface Wambura
Ofisa Habari
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)
Mjumbe, Kamati ya Habari CECAFA

0 Weka maoni yako hapa:

Post a Comment

COMMENT HAPA