May 4, 2013

AZAM KUSHUKA DIMBANI LEO SAA MOJA USIKU


 

Azam FC leo inatupa karata yake ya sita kwenye michuano ya CAF Confederations Cup huku ikiwa na rekodi ya kucheza michezo mitano tayari pasi na kupoteza hata mmoja. ikumbukwe kuwa tangia kuumbwa kwa taifa la Tanzania hakuna klabu ya soka iliyowahi kucheza zaidi ya michezo mitano pasi na kupoteza hata mmoja zaidi ya Azam FC na Simba SC mwaka 1993. Azam FC ikishinda au kutoka sare leo itakuwa imevuka rekodi hiyo huku ikiwa inawakilisha nchi kwa mara ya kwanza.

Katika makala mbili za nyuma tulijadili sababu sita kwa nini Azam FC leo ina nafasi ya kushinda mchezo huu, katika mjadala huo kipengele pekee ambacho hatukukimalizia ni wasifu wa washambuliaji wetu.
Hapa tutawaletea dondoo kuhusu washambuliaji wanaotarajia kuongoza safu ya ushambuliaji ya Azam FC hii leo.

Kipre Tchetche, Khamis Mcha Viali na Braian Umony ndiyo washambuliaji wa pembeni ambao mwalimu Stewart Hall atalazimika kuchagua wawili ili kuanza leo huku John Bocco akicheza katikati hiyo leo… lakini Azam FC inao viungo wengine wa pembeni na washambuliaji ambao imesafiri nao kama Uhuru Selemani, Abdallah Seif karihe na Gaudence Mwaikimba.

Kwa jinsi timu inavyocheza mazoezini, ni wazi kuwa John Bocco atasimama katikati akipewa sapoti na Kipre Tchetche na Brian Umony. Watatu hawa ni wachezaji wa kiwango cha juu sana kwa sasa. Umony ni mchezajo bora wa CECAFA Challenge Cup. Bocco ni mfungaji bora wa Ligi Kuu Tanzania Msimu uliopita na CECAFA Challenge Cup huku Kipre Tchetche akiwa mfungaji bora wa msimu huu ligi kuu Tanzania.

Unapokuwa na wachezaji wenye sifa hizi huku kwenye benchi ukiwa na akiba ya watu kama Uhuru Selemani, Abdallah Seif karihe, Khamis Mcha Viali wa Unguja na Gaudence Mwaikimba unapata nini zaidi ya ushindi?
Ni dhahiri kuwa unapokuwa na kikosi kama hiki lazima utajiamini.

Kocha Stewart Hall anaweza kuwapanga khamis Mcha na Kipre Tchetche pembeni mwa Bocco… ama anaweza kuwaanzisha Brian Umony na Kipre Tchetche pembeni mwa Bocco machaguo hayo mawili yatampa aina tofauti za kushambulia na kulinda goli.

Mcha Khamis Viali yeye ni mzuri sana kwenye kukaba na aina yake ya kushambulia ni ya kipekee kabisa kiasi kwamba ni vigumu kumdhibiti. Mcha hucheza na nafasi, hapotezi muda na mpira na anapoingia kwenye eneo la kufunga basi hupasia mpira kambani kwa utulivu.

Ukimuangalia alivyo usoni huwezi kudhani kuwa anaweza kuwa na madhara lakini awapo uwanjani ni mchezaji aliyekamilika. Ana balance, anajua kumiliki mpira, miguu yake ina macho na anajua kusoma ramani ya namna mchezo unavyokwenda na jinsi gani aifanyie kazi.

Ukiachana na Mcha, Kipre Tchetche yeye kwa sasa ni “Deadly Killer”… Kipre anapokuwa na mpira wapinzani wanapata homa, chenga zake anapowatoroka mabeki huwafanya makae chini na anapofika kwenye eneo la adui huwa hana masihara. Kutamba kote kwa Azam FC kunatokana na kuwana na nyota huyu wa Ivory Coast ambaye ana miaka miwili sasa tangia atue Azam FC.

Brian Umony ambaye alitamba na Uganda Cranes kama mshambuliaji wa kati sasa amehamishiwa pembeni na spidi yake anaposhambulia na akili nyingi alizonazo anapoichambua kama karanga ngome ya maadui ndiyo silaha kuu inayotegemewa na Azam FC hapo leo.

Brian ambaye amekuwa akisumbuliwa na majeruhi kwa muda mrefu kwa sasa yupo fiti 100% na inshallah kama atapata nafasi ya kuanza tutarajie makubwa toka kwake.
Kwa mashabiki wa ukweli wa Azam FC huhitaji kumuelezea John Bocco, Bocco anapokuwa majeruhi basi Azam FC hupooza na kwa sasa nahodha huyu anaonekana kuwa si kiongozi wa wachezaji wenzake tuu kama nahodha bali pia roho ya klabu.

John Bocco ana nguvu sana na anajua kucheza kama screen man akiwafanya wapinzani wamuwekee ulinzi wa watu watutu hivyo kutoa mwanya kwa wenzake kucheza.

Unaweza ukadhani Bocco hachezi vizuri anapotimiza majukumu yake… lakini matokeo ya mwisho ya ushindi ndiyo yatakayokupa majibu. Timu nyingi huingia kwenye mtego wa John Bocco wa kucheza naye kidali poo na kufukuzana bila mpira huku Kipre Tcheche na wenzake wakifanya mambo na kuipa Azam FC ushindi. Ngoja tuone nini kitatokea.

Timu leo huenda ikapangwa kama ifuatavyo

Mwadini Ally Mwadini (GK)
Himid Mao Mkami (RB)
Waziri Salum Omar (LB)
David John Mwantika (CB)
Jockins Atudo (CB)
Kipre Bolou Michael (MF)
Salum Abubakar (MF)
Humphrey Mieno(MF)
Kipre Tchetche Herman (RW)
John Bocco (STR)
Brian Umony (LW)Azam FC


wakati huo huo