Dec 23, 2013

YANGA YASITISHA MKATABA NA BRANDTS

  Mwenyekiti wa Kamati ya Mashindano Abdallah Bin Kleb (katikati) akiongea na waandishi wa habari makao makuu ya klabu ya Yanga, kushoto ni Musa Katabaro na kulia Afisa Habari Baraka Kiziuguto

Uongozi wa klabu ya Young Africans SC umempatia taarifa (Notice) ya siku ya thelathini (30) kocha mkuu mholanzi Ernie Brandts juu ya kusitisha mkataba wake kuanzia jana Disemba 22 mwaka huu.
 
Maamuzi hayo yanafuatia muenendo wa matokeo mabaya katika michezo iliyopita ya Ligi Kuu, kirafiki na bonanza la Nani Mtani Jembe dhidi ya Simba SC mwishoni mwa wiki.
 
Hatua ya Young Africans SC kusitisha huduma na Brandts isichukuliwe kama chuki bali ni moja ya sehemu ya kuhakikisha tunaboresha benchi la ufundi ili tuweze kupata matokeo mazuri katika Mashindano yanayotukabili.
 
Ukitazama uwezo wa mchezaji mmoja mmoja wa Yanga SC na wapinzani wetu, na soka tulilocheza kwenye mchezo wa mwishoni mwa wiki kwa kweli ni dhahiri mwalimu amefikia mwisho kimbinu na hana njia mbadala.
 
Young Africans SC imekua ikicheza chini ya kiwango katika michezo ya Ligi Kuu hali iliyoplekea kupata ushindi kwa tabu na wakati mwingine timu kupoteza pointi.
 
Kufuatia kupewa taarifa ya siku 30, Brandts ataamua mwenyewe kama ataendelea kusimamia mazoezi ya timu au kuondoka moja kwa moja kabla ya muda huo ukiwa haujakamilika.
 
Ikiwa Brandts ataondoka mapema timu itaendelea na mazoezi kama kawaida katika kila siku asubuhi katika uwanja wa bora kijitonyama kujiandaa na mzunguko wa pili wa Ligi Kuu na mashindano ya kimataifa chini ya kocha msaidizi Fred Felix “Minziro”.
 
Ili kuhakikisha timu inafanya vizuri katika mzunguko wa pili wa Ligi Kuu ya Vodacom na mashindano ya kimataifa uongozi unakamilisha maandalizi ya safari ya kambi nje ya nchi na taratibu zote zitakapokamilika tutawajulisha.
 
Aidha uongozi upo katika mchakato wa kumapata mrithi wa Brandts ambaye ataungana na timu kwa ajili ya maandalizi ya mzunguko wa pili na Mashindano ya klabu Bingwa Afrika.
 
Mwisho tunawaomba wanachama, wapenzi na washabiki wa Yanga wasivunjike moyo kufuatia matokeo ya bonanza mwishoni mwa wiki, uongozi unajipanga kuhakikisha timu inaimarika kwenye benchi la ufundi na kurudisha furaha katika mzunguko wa pili wa VPL.


Abdallah Bin Kleb
Mwenyekiti - Kamati ya Mashindano
Young Africans Sports Club.

DAR ES SALAAM
23 Disemba, 2013
 

0 Weka maoni yako hapa:

Post a Comment

COMMENT HAPA