Jun 12, 2012

TFF: Yondani atacheza Yanga 100%




LAMPS COLLIN
UTATA wa usajili wa Kelvin Yondani unaelekea kupata majibu mapema baada ya kuthibitika kuwa ataichezea Yanga msimu ujao.

Mmoja wa wajumbe wa kamati mmojawapo ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) aliithibitishia Mwanaspoti jana Jumatatu kuwa Yondani atacheza Yanga msimu ujao baada ya kugundua udanganyifu uliofanyika Simba.

"Hapa tuwe wa kweli. Simba wanasema walimsainisha Yondani Desemba mwaka jana, tunajua kuwa Yondani alikuwa na matatizo na Simba wakati huo angesaini vipi mkataba mpya?" Alihoji mjumbe huyo wa TFF.

Mjumbe huyo alisema Simba wanaonekana kushindwa mapema katika kesi hiyo kwa sababu kama wangekuwa wanamtaka Yondani wangemsainisha kabla hajaingia miezi sita ya mwisho na mkataba wake ungesajiliwa TFF.

"Hivi unadhani Simba wangekuwa wanamtaka Yondani wangesubiri mpaka mkataba wake uishe?" Alihoji.

"Huyu sisi tuna taarifa kuwa alisaini Simba baada ya timu kurejea kutoka Algeria katika Kombe la Shirikisho. Ila walichokifanya ni kurudisha nyuma tarehe ya usajili ili ionekane amesajili Desemba.

"Hata kama amesajili Desemba bado walichelewa kwa sababu wakati huo tayari Yondani alikuwa amebakiza mkataba wa miezi sita, hivyo alikuwa huru kusaini klabu yoyote. "

Mwanaspoti ilipomuuliza Yondani atacheza timu gani msimu ujao alisema: "Kwa mazingira yote hayo ni dhahiri atacheza Yanga kwa asilimia mia."

Familia ya Yondani
Kaka mkubwa wa Kelvin Yondani ambaye pia ni wakala wa mchezaji huyo, Sunday Patrick ameridhia beki huyo kwenda Jangwani.

Sunday aliiambia Mwanaspoti wiki iliyopita kuwa: "Sisi kama familia kwa moyo mmoja tupo na Yondani katika uamuzi wake, cha msingi yeye amefuata sheria na hana mkataba wowote na Simba ndio maana hata sisi tumempa baraka za kwenda Yanga, pia viongozi wa Simba wanapaswa kufahamu kuwa mchezaji huyu bado ni mdogo na anatafuta maisha hivyo wamuache afanye uamuzi wake."

Kauli ya Yondani
Yondani ambaye awali alidai kusaini Simba, Alhamisi iliyopita aliikana kauli hiyo na kusema amesaini Yanga.
"Nimesaini Yanga, nawatakia kila la kheri Simba."

Yondani amelamba Sh.30 milioni kutoka Yanga na atakuwa akilipwa mshahara wa Sh 800,000 ingawa kuna taarifa kuwa ameongezewa na atakuwa akilipwa Sh milioni moja kwa mwezi huku ikidaiwa Simba ilipanga kumpa Sh 25 milioni na angelipwa mshahara wa Sh 800,000.

Kanuni ya TFF
Kanuni ya 43 ya TFF ya masharti ya mikataba kati ya wachezaji na klabu kifungu cha 3 kinasema; " Klabu inayotarajia kuingia mkataba na mchezaji wa kulipwa haina budi kuiarifu klabu yake ya sasa kwa maandishi kabla ya kufanya makubaliano na mchezaji huyo wa kulipwa.

Mchezaji wa kulipwa atakuwa huru tu kuingia mkataba na klabu nyingine iwapo mkataba wake na klabu yake ya sasa umekwisha au utakwisha baada ya miezi sita. Uvunjaji wowote wa sharti hili utastahili vikwazo vinavyofaa."

Tafsiri ya kanuni
Kutokana na kanuni hiyo, Yondani alikuwa huru kufanya mazungumzo au hata kusaini mkataba na klabu yoyote tangu Desemba mwaka jana kwa sababu mkataba wake ulikuwa umebakiza miezi sita kwani umekwisha Mei 31 mwaka huu.


chanzo na http://www.mwanaspoti.co.tz                                                                 

0 Weka maoni yako hapa:

Post a Comment

COMMENT HAPA