Nov 8, 2013

Sheikh Ponda Kuendelea Kusota Rumande Hadi Nov 21



KESI yenye mashtaka matatu inayomkabili Katibu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu nchini, Sheikh Ponda Issa Ponda, katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Morogoro, imeshindwa kusikilizwa baada ya jalada halisi la kesi hiyo kuitishwa katika Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam kwa ajili ya kupitiwa upya.

Sheikh Ponda alifikishwa mahakamani hapo jana asubuhi kwa kutumia usafiri wa basi maalumu la Magereza na safari hii kesi yake ilikuwa mbele ya Hakimu Mkazi Mwandamizi, Mary Moyo, baada ya hakimu aliyekuwa akisikiliza tangu awali, Richard Kabate, kuhamishiwa mkoani Dodoma.

 Akitoa maelezo ya kesi hiyo, Hakimu Moyo alisema kuwa jalada halisi la kesi hiyo limeitishwa Mahakama Kuu Dar es Salaam Oktoba 15, mwaka huu, kwa ajili ya mapitio na kwamba Mahakama Kuu ina mamlaka ya kisheria ya kuitisha jalada, hivyo kesi hiyo haitaweza kusikilizwa hadi litakaporudi.

 Hakimu Moyo alisema kuwa kwa sasa kesi hiyo itakuwa ikitajwa tu na suala la mshitakiwa kuletwa ama kutoletwa mahakamani liko chini ya Magereza, kwani dhamana ya mshitakiwa huyo imefungwa, hivyo ataendelea kuwepo gerezani hadi Novemba 21, mwaka huu, itakapotajwa tena mahakamani hapo. 

Mapema baada ya kufikishwa mahakamani hapo, Hakimu Moyo alimuuliza Sheikh Ponda kama ana taarifa zozote kuhusu kutokufika kwa mawakili wake watatu ambao ni Batholomew Tarimo, Ignas Punge na Juma Nassor, hata hivyo Sheikh Ponda alidai kuwa hana taarifa zozote.

Hata hivyo, upande wa mashtaka ukiongozwa na Wakili wa Serikali, Sunday Hyela, umedai kuwa uko tayari kutoa ushahidi ambao ungeanza na askari polisi mwenye namba F 4949 DC Kingazi wa Kituo Kikuu, lakini hakuweza kutoa ushahidi wake kutokana na jalada halisi la kesi hiyo kuitishwa na Mahakama Kuu kwa ajili ya mapitio.

0 Weka maoni yako hapa:

Post a Comment

COMMENT HAPA