Mar 7, 2014

Kampuni itakayoshughulikia kumuenzi marehemu Steven Kanumba kuzinduliwa mwezi ujao

 


Uzinduzi wa taasisi ya marehemu Steven Kanumba ijulikanayo  kwa jina la Kanumba The Great Foundation utafanyika Aprili 7 kwenye ukumbi maarufu wa Dar Live uliopo Mbagala, jijini.

 Uzinduzi huo utaenda sambamba na maadhimisho ya miaka miwili tokea kufariki kwa marehemu Kanumba ambaye alifariki dunia Aprili 7.

Akizungumza na waandishi wa habari jana, Mama mzazi wa marehemu Kanumba, Flora Mtegoa alisema kuwa wameamua  kuanzisha taasisi hiyo ili kuendelea kumuenzi mtoto wake na kuendeleza kile ambacho alikuwa akikifanya wakati wa uhai wake.

Alisema kuwa taasisi yao itajihusisha na utoaji wa elimu, kusaidia watoto yatima, kuibua vipaji vya waigizaji chipukizi na kuviendeleza na mambo mbali mbali ya jamii na tasnia ya filamu na muziki.

“Kwa njia hii, jamii itaendelea kumkumbuka kila siku na si kusubiri maadhimisho ya siku yake aliyokufa tu, siku hii (Aprili 7 kila mwaka) itabaki kuwa ya kukumbukwa, lakini tutajihusisha na mambo mengine ya maendeleo na kusaidia jamii,” alisema Mtegoa.

Alisema kuwa wameamua kuipa jukumu kampuni ya Vannedrick  Tanzania Limited kufanya shughuli za uzinduzi wa taasisi hiyo kutokana na uadilifu wao na kuvunia na jinsi inavyojihusisha na mambo mbali mbali katika jamii.

Mkurugenzi kuu wa Vannedrick Tanzania Limited Frederick Mwakalebela alisema kuwa siku hiyo mbali ya kuwa na Red Carpet, pia kutakuwa na burudani mbali mbali za muziki wa dansi, muziki wa kizazi kipya na vichekesho kutoka kwa wasanii maarufu hapa nchini.

Alisema kuwa kutakuwa na maonyesho ya filamu mbali mbali za marehemu Kanumba ikiwa pamoja na script alizokuwa akiandika yeye mwenyewe, nyimbo alizotunga na vingienvyo.

“Pia kutakuwa na burudani kutoka kwa wasanii wa Bongo Movie ambao wameanza maandalizi kwa ajili ya siku hiyo maalum kwa waigizaji na mashabiki wa filamu nchini, tunawamba wadhamini wajitokeze ili kufanikisha siku hiyo,” alisema.

 



0 Weka maoni yako hapa:

Post a Comment

COMMENT HAPA