Jul 31, 2014

TAMKO LA UKAWA KUHUSU WITO WA VIONGOZI WA DINI WA KURUDI BUNGENI



UKAWA WAIJIBU BAKWATA

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI,
DAR ES SALAAM, ALHAMISI, 31 JULAI 2014 SAA 5.00ASUBUHI

TAMKO LA UKAWA KUHUSU WITO WA VIONGOZI WA DINI WA KURUDI BUNGENI

Ndugu waandishi wa habari,

Kama mnavyofahamu Wajumbe wa Bunge Maalum la Katiba (BMK) wanaotetea kuheshimiwa kwa maoni ya Wananchi katika mchakato wa kuandika Katiba maarufu kwa jina la UKAWA- Umoja wa Katiba ya Wananchi walitoka nje ya Bunge hilo tarehe 16 April 2014.

Sababu ya msingi iliyotutoa kwenye BMK ni mkakati uliokuwa ukitekelezwa na Wajumbe wa BMK wa CCM kupuuza maoni ya wananchi yaliyokusanywa na kuratibiwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba ikiongozwa na Mwenyekiti Jaji Joseph Sinde Warioba na Makamu mwenyekiti Jaji Agostino Ramadhani.

Rasimu ya Katiba inapendekeza Muundo wa Muungano wa Shirikisho yenye Serikali Tatu. Kama waraka wa CCM unavyoeleza “Muundo wa Muungano ndiyo moyo wa Rasimu na ndiyo unaoamua ibara nyingine zikae vipi.” CCM wameukataa Muundo wa Muungano uliopendekezwa na Tume, na badala yake wanataka Muundo wa Serikali mbili ambao haujafanyiwa utafiti, haujapendekezwa na wananchi walio wengi, uliojaa na matattizo lukuki yasiyotatulika tangu enzi za uhuru na ambao haujapendekezwa na tume ya mabadiliko ya katiba.

Kwa sababu aina ya muundo wa muungano ndiyo moyo wa rasimu ya katiba(kwa tafsiri ya CCM), ukiunyonga Moyo wa Rasimu hautakuwa na Rasimu ya Katiba inayotokana na maoni ya wananchi. UKAWA tunatetea maoni ya Wananchi yaheshimiwe na tumetoa wito kila mara kuwa hii ndiyo njia bora ya kutufanya turidhiane.

Ikumbukwe kuwa bunge la katiba halikuanzisha mchakato wa katiba, linakamilisha moja ya hatua muhimu za kupata katiba, tayari hatua mbili muhimu zimeshafanyika, maoni ya wananchi yametolewa na tume imetumia maoni hayo pamoja na rejea zingine na historia mbalimbali na imetuletea Rasimu ya Katiba inayotokana na mambo hayo. Bunge Maalum la Katiba halina uwezo na kibali cha kuvunja misingi mikuu ya maoni ya wananchi na kazi ya tume.

Kuvunja misingi mikuu “moyo wa rasimu” ni sawa na kuanzisha mchakato mwingine wa katiba na ni sawa na kuwa juu ya maoni na matakwa ya wananchi. UKAWA tumekataa kuwa sehemu ya uchakachuaji huu wa hali ya juu.

Ndugu waandishi wa habari,

Tunapenda ifahamike kuwa, UKAWA pia tulikwazwa na lugha za ubaguzi, uchochezi, matusi na kejeli zilizokuwa zikiporomoshwa na baadhi ya Wajumbe wa CCM ndani na nje ya BMK. Michango mingi ya Wajumbe wa CCM wa Bunge Maalum ilikuwa ya kumkejeli na kumdhalilisha Jaji Joseph Sinde Warioba na kauli za kibaguzi dhidi ya Waarabu, Wapemba na Wahindi.

Lugha za kibaguzi na kichochezi pia zilitolewa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera Uratibu na Bunge), William Lukuvi alipokuwa anamwakilisha Waziri Mkuu Mizengo Pinda katika ibada ya kumsimika Askofu wa Kanisa la Methodist, Jimbo la Dodoma.

Mhe. Lukuvi aliwataka wananchi waliohudhuria ibada hiyo kupinga serikali tatu zilizopendekezwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba, vinginevyo nchi itatawaliwa na jeshi kwa kuwa Serikali ya Muungano itashindwa kuwalipa mishahara wanajeshi. Katika hotuba yake katika kanisa la Methodist Mhe. Lukuvi aliendelea kuwachochea waumini aliposema kuwa “Serikali tatu zikipita ni wazi kuwa hata makanisa yatafungwa kwani nchi haiwezi kuwa na amani tena.”

Lukuvi alisema Wazanzibari wanaotaka kuwa na nchi yao hawawezi kujitegemea, bali wanataka Serikali ili wapate nafasi ya kujitangaza kuwa ni nchi ya Kiislamu. Serikali haikuchukua hatua yeyote kukanusha na kumuwajibisha Mhe. Lukuvi.

Hivi karibuni kumekuwa na miito mbalimbali ambayo imetolewa kututaka sisi tulioko katika Umoja wa Kutetea Katiba ya Wananchi (UKAWA), kurejea bungeni. Katika Baraza la IDD ambako Waziri Mkuu Mizengo Pinda alikuwa mgeni rasmi wito wa UKAWA kurudi bungeni ulisisitizwa.

Watu wengi wametoa kauli na hasa baadhi ya viongozi wa madhehebu mbalimbali ya kidini nchini, kututaka turejee bungeni ili kuendelea na mchakato wa kuandika katiba mpya. Tunasema, tumewasikia na tunaheshimu kauli zao.

Tunatambua kuwa viongozi wa kidini ni watu wenye heshima na nafasi ya pekee katika jamii yetu. Ni watu waliopewa wajibu wa kutuongoza tukiwa hapa duniani na hata tukiondoka duniani. Kwa hiyo, napenda kuwahakikishieni kabisa kuwa UKAWA inaheshimu sana miito na ushauri wao.

Ndugu waandishi wa habari,

Pamoja na heshima hiyo, tunapenda pia waelewe haya yafuatayo:
Kwanza, UKAWA uliondoka bungeni, pamoja na mengine, kupinga njama za kuhujumu mchakato wa Katiba Mpya. Tulipinga kudharauliwa maoni ya wananchi kama yalivyowasilishwa bungeni na Mwenyekiti wa Tume ya Rais ya Mabadiliko ya Katiba, waziri mkuu mstaafu, Jaji Joseph Sinde Warioba.

Tumepinga Chama Cha Mapinduzi (CCM), kupuuza maoni ya wananchi na kutaka kuingiza maoni yake, kinyume cha kanuni na Sheria ya Mabadiliko ya Katiba.

Pili, tuliondoka bungeni kupinga lugha ya ubaguzi, uchochezi, matusi na kejeli. Baadhi ya kauli hizi tulizikabili ndani ya bunge na kuonya wenzetu kuacha lugha hizo na badala yake watumie jukwaa hilo kusaidia upatikanaji wa katiba mpya. Hatukusikilizwa.

Ninyi ni mashahidi jinsi wajumbe wa CCM walivyoporomosha matusi makubwa na tuhuma nzito dhidi ya Tume ya Jaji Warioba. Baadhi ya wajumbe waliwaita wajumbe wa tume hii Eti, “wasaliti wa Baba wa Taifa; wazee wanaosubiri kufa; na watu wasiokuwa na uzalendo bali wana ajenda binafsi.”

Tatu, tuliondoka bungeni baada ya Mwenyekiti wa Bunge la Katiba, Mhe. Samuel Sitta kushindwa kuwadhibiti wajumbe wanaotumia lugha ya ubaguzi, uchochezi, matusi na kejeli na kuendesha vikao vya bunge hilo kwa upendeleo.

Mwenyekiti ameliendesha Bunge hilo kibabe. Ameshiriki kubadili ratiba na mtiririko wa matukio bungeni. Mwenyekiti wa Bunge la Katiba alivunja kanuni kwa kumtanguliza Mwenyekiti wa Tume kuwasilisha Rasimu kabla Bunge kusikiliza hotuba ya ufunguzi ya Mgeni Rasmi. Amebadili Kanuni za Bunge la Katiba na sasa ametishia kufanya hivyo tena.

Nne, tuliondoka bungeni baada ya kuona waziri mmoja mwandamizi wa serikali ya Rais Kikwete, William Lukuvi, akiingia kanisani na kufanya uchochezi. Alidai Zanzibar inataka serikali tatu ili iwe huru kuanzisha Serikali ya Kiislamu na kuwarejesha Waraabu visiwani humo.

Waziri huyu alikuwa amekwenda Kanisani kumwakilisha Waziri Mkuu, Mizengo Pinda. Hadi tunaondoka na mpaka sasa, hakuna mamlaka yoyote iliyo juu ya Lukuvi ambayo imechukua hatua angalau hata ya kuomba radhi. Waziri Mkuu alikuwa na fursa adhimu kama mgeni rasmi katika Baraza la Idd kuomba radhi lakini hakufanya hivyo.

Tunawashukuru sana viongozi wa dini waliotoa matamko kulitaka Bunge Maalum la Katiba liheshimu maoni ya wananchi.

Ndugu waandishi wa habari,

Pamoja na kuwaheshimu viongozi wote wa dini, tumesikitishwa na matamshi ya baadhi yao kama yale yaliyotolewa katika Baraza la Idd kututaka UKAWA turejee bungeni, huku wakinyamazia matendo yaliyofanyika. Waziri Mkuu aliyekuwa mgeni rasmi katika Baraza la Idd ndiye aliyewakilishwa na Waziri Lukuvi alipotoa alipotoa kauli za kibaguzi na kichochezi katika kanisa la Methodist mjini Dodoma.

Leo ni zaidi ya miezi miwili tangu Bunge hili liahirishwe. Hatujamsikia kiongozi yoyote wa kidini (wale) wanaotutaka turudi bungeni, wakikemea au kutoa wito kwa Mwenyekiti wa Bunge Maalum kutumia haki, hekima na usawa, katika kuendesha mijadala bungeni.

Hatujasikia viongozi wa dini wanaotaka UKAWA warudi Bungeni wakitoa wito kwa wabunge wa chama tawala kurejea kwenye ajenda kuu na kuacha kashfa dhidi ya Tume. Kimya chao katika suala hili, kimechangia kukiongezea chama tawala kibri na dharau dhidi ya wananchi.

Vilevile, hatujawasikia viongozi wa madhehebu ya kidini wakimkemea Lukuvi wala Waziri Mkuu Pinda kuhusu kilichotokea kanisani Dodoma.

Badala yake, tumeendelea kuona viongozi wa dini wakikutana na viongozi wa serikali na chama tawala, bila jitihada za viongozi hao kukutana na UKAWA. Miito ya viongozi hawa inaelekezwa upande mmoja ikifumbia macho upande wa pili.

Sisi tunaamini viongozi wetu wa kiroho wanao uwezo wa kuangalia pande zote mbili na kutoa miito yenye ukweli, usawa na haki.

Tunawasishi kabla ya kututaka kurejea bungeni, wangetumia busara hiyohiyo kutusikiliza na sisi kama ambavyo wanawasikiliza viongozi wa CCM.

Msimamo wa UKAWA uko wazi, tunataka maoni ya wananchi yaheshimiwe na Bunge Maalum la Katiba.
Mungu Ibariki Tanzania!
Imetolewa na;

-----------------------------------
Freeman Alkael Mbowe(MB),
Mwenyekiti - CHADEMA

---------------------------------------
Ibrahim Haruna Lipumba(MBMK)
Mwenyekiti – CUF – Chama Cha Wananchi,

--------------------------------------
James Francis Mbatia(MB)
Mwenyekiti – NCCR MAGEUZI.

0 Weka maoni yako hapa:

Post a Comment

COMMENT HAPA