Nov 11, 2013

LIPUMBA ASHAURI TANZANIA TUJIPANGE KUIMARISHA UCHUMI WETU NDANI YA JUMUIYA YA AFRIKA MSHARIKI.

  

THE CIVIC UNITED FRONT - CUF,

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI - Na. Prof Ibrahim Lipumba,

TAREHE 10/11/2013

TANZANIA TUJIPANGE KUIMARISHA UCHUMI WETU NDANI YA JUMUIYA YA AFRIKA MSHARIKI.

Tarehe 7 Novemba 2013 Rais Kikwete alilihutubia Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Madhumuni makubwa ya hotuba hiyo ilikuwa kuelezea msimamo wa Tanzania kuhusu Jumuiya ya Afrika Mashariki baada ya Kenya, Uganda na Rwanda kukutana mara tatu bila kuihusisha Tanzania. Katika mikutano ya viongozi wakuu wa nchi hizo ambayo iliishirikisha Sudan ya Kusini walijadili na kufikia maazimio kuhusu mambo ambayo kimsingi na kiitifaki yanapaswa kujadiliwa katika vikao vya Jumuiya ya Afrika Mashariki.

CUF – Chama Cha Wananchi kinaunga mkono msimamo wa Rais Kikwete kuwa pamoja na vitimbi vilivyofanywa na Kenya, Uganda na Rwanda dhidi ya Tanzania na Burundi, Tanzania haitajitoa na wala haitakuwa chanzo cha kuvunjika kwa Jumuiya ya Afrika Mashariki. CUF inalaani vikali vitimbi vya kuitenga Tanzania vilivyofanywa na Kenya, Uganda na Rwanda. Tunatoa wito kwa Watanzania wote kushikamana kwa dhati, kujenga umoja wa kitaifa, kujenga na kuimarisha miundombinu ya nchi yetu na kuongeza ushindani wetu wa kiuchumi ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki na Ulimwengu kwa ujumla.

Tarehe 24-25 Juni 2013, siku chache kabla Rais Obama hajatua Dar es Salaam, Marais wa Kenya, Rwanda na Uganda walikutana kuimarisha uhusiano wao wa kibiashara na kurahisisha usafiri baina ya nchi hizo tatu. Kwa kawaida masuala haya ya kuimarisha biashara na usafiri baina ya nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki huzungumzwa kwa pamoja na nchi zote wanachama wa Jumuiya hii. Inaelekea Kenya, Rwanda na Uganda wameamua kuwaacha kando Tanzania na Burundi.

Mimi nilidhani ziara ya Rais Obama Tanzania ilielekea kutowafurahisha baadhi ya jirani zetu ambao wangependa Rais Obama atembelee nchi zao badala ya Tanzania. Kenya walisusia Mkutano wa Rais Obama na Wafanyabiashara wa Africa (Business Leaders Forum) ambao uliandaliwa na Corporate Council on Africa.

Uhusiano kati ya Rwanda na Tanzania umezorota baada ya Rais Kikwete kuwapa ushauri viongozi wenzake katika kikao cha Umoja wa Afrika, Addis Ababa kuwa njia muhimu ya kumaliza migogoro ya kisiasa na kiusalama na kuleta amani katika Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo ni kwa nchi jirani za Kongo, ikiwemo Rwanda na Uganda ni kuzungumza na kufikia muafaka wa kisiasa na mahasimu na waasi wao waliokimbilia Kongo. Ushauri wa Rais Kikwete umetafsiriwa visivyo nchini Rwanda na kusababisha kuzorota kwa uhusiano kati ya nchi zetu mbili.

Wachambuzi wa mambo ya uhusiano wa kimataifa wanaamini ushauri wa Rais Kikwete umechukuliwa kama kisingiziyo. Tatizo kubwa ni Tanzania kukubali kupeleka wanajeshi wake Kongo kama sehemu ya Jeshi la Umoja wa Mataifa la kuleta amani Mashariki ya Kongo. Wanajeshi wetu ndani ya Brigedi Maalum ya Jeshi la Umoja wa Mataifa Kongo (MONUSCO) inayoongozwa na Brigedia Jenerali James Aloisi Mwakibolwa wa JWTZ imefanya kazi nzuri na kufanikisha kulisaidia Jeshi la Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo kulisambaratisha jeshi la waasi la M23 ambao viongozi wake wa juu wamekimbilia Uganda.

Tarehe 28 Agosti, 2013 viongozi wa Kenya, Uganda na Rwanda walikutana mjini Mombasa, Kenya ambapo walishiriki katika sherehe maalum ya Rais Kenyatta kuzindua gati jipya la kuegesha meli ili ziweze kupakuliwa kwa haraka na kuongeza ufanisi. Lengo la Mamlaka ya Bandari ya Kenya ni kuifanya Mombasa kuwa bandari inayoongoza kwa kuhudumia siyo tu Kenya, bali Tanzania ya Kaskazini, Uganda, Rwanda, Burundi, Kongo, Sudan ya Kusini, Ethiopia na Somalia.

Mkutano wa tatu wa Marais wa Kenya, Uganda na Rwanda ulifanyika tarehe 28 Oktoba, 2013 mjini Kigali, Rwanda. Rais Kikwete ameeleza kuwa Mambo yapatayo manane ya msingi yaliyoamuliwa kufanywa na nchi hizo;

(1) Kujenga reli ya kisasa kutoka Mombasa hadi Kampala, Kigali na Bujumbura.

(2) Ujenzi wa Bomba la Mafuta la kutoka Kenya hadi Uganda na Sudani ya Kusini.

(3) Kujenga Kiwanda cha kusafisha mafuta nchini Uganda.

(4) Kuanzisha Himaya Moja ya Ushuru wa Forodha wa Jumuiya ya Afrika Mashariki na kutekeleza vipengele vyote;

(5) Kuharakisha Shirikisho la Afrika Mashariki na kwamba itaundwa Kamati ya kuandaa rasimu ya Katiba ya Shirikisho.

(6) Kuharakisha uanzishwaji wa Visa ya pamoja ya Utalii ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (Single East African Community Tourist Visa);

(7) Kuandaa utaratibu wa kutumia vitambulisho vya taifa kama hati ya kusafiria katika nchi zao; na

(8) Kuongeza uzalishaji na usambazaji wa umeme.
Katika mambo haya manane, manne yanatawaliwa na itifaki ya Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Mambo hayo manne ni Kuanzisha Himaya Moja ya Ushuru wa Forodha wa Jumuiya ya Afrika Mashariki na kutekeleza vipengele vyote, Kuharakisha Shirikisho la Afrika Mashariki, Kuharakisha uanzishwaji wa Visa ya pamoja ya Utalii ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, Kuandaa utaratibu wa kutumia vitambulisho vya taifa kama hati ya kusafiria.

Katika haya manne Rais alieleza kuwa mawili yalifanyiwa uamuzi wa pamoja na hana matatizo nayo. “Mambo hayo ni matumizi ya vitambulisho vya taifa kama hati ya kusafiria na Visa ya Pamoja ya Utalii kwani tuliamua kwa pamoja kuwa nchi wanachama zilizokuwa tayari waanze.”

Katika masuala ya kuanzishwa kwa Himaya Moja ya Ushuru wa Forodha (Single Customs Territory) na Shirikisho la Afrika Mashariki Kenya, Uganda na Rwanda wamekiuka uamuzi wa pamoja wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Rais alieleza “Katika Mkutano Maalum wa 11 wa Wakuu wa Nchi wanachama uliofanyika tarehe 28 Aprili, 2012 Jijini Arusha, tulipokea na kuridhia mapendekezo ya kuanzisha Himaya Moja ya Ushuru wa Forodha (Single Customs Territory).

Kwa mujibu wa mapendekezo hayo kila nchi mwanachama itasimamia shughuli zake za kiforodha na kukusanya mapato yake kama ilivyo sasa. Hata hivyo, kwa bidhaa zinazopitia nchi moja kwenda nchi nyingine mwanachama, ukaguzi na ukusanyaji wa mapato utafanyika katika kituo cha kwanza bidhaa hizo zinapoingilia.

Mapato hayo yatawasilishwa kwa nchi husika baada ya kuthibitisha kuwa bidhaa zilivuka mpaka. Wakuu wa Nchi waliagiza Baraza la Mawaziri kuunda Kikosi Kazi cha kujadiliana na kuandaa utaratibu wa utekelezaji wa mfumo huo.

Taarifa ya kikosi kazi inatakiwa kutolewa katika Mkutano wa 15 wa Wakuu wa Nchi utakaofanyika Kampala, Uganda tarehe 30 Novemba, 2013. Kabla hata ya kupokea taarifa ya kikosi kazi, Kenya, Uganda na Rwanda wameamua kutekeleza Single Customs Territory nje ya taratibu za Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Mwezi Agosti Chama cha Wasafirishaji wa Mafuta Tanzania (Tatoa) kilitoa taarifa kwenye Kamati ya Kudumu ya Bunge inayosimamia mambo ya Bajeti kuwa ifikapo Septemba mwaka huu Rwanda na Uganda watasitisha kutumia bandari ya Dar es Salaam kupitisha mizigo yao. Serikali ilikanusha taarifa lakini inaonekana kuwa Rwanda na Uganda wameamua kuwa watasita kutumia bandari ya Dar es Salaam na kwa hiyo wanaweza kuanzisha taratibu za Single Customs Territory na Kenya bila kuishirikisha Tanzania.

Taarifa kuhusu Rwanda na Uganda, kutotumia Bandari ya Dar es Salaam lisitazamwe kisiasa. Bandari ya Dar es Salaam ina udhaifu mkubwa unaolalamikiwa na wafanyabiashara wa ndani na nje ya nchi. Siyo Rwanda na Uganda tu ndiyo wanaoilalamikia bandari ya Dar es Salaam, bali Kongo, Zambia na Malawi pia wanalalamika.

Bandari ya Dar es Salaam ina sifa ya ucheleweshaji wa kupakua shehena za mizigo toka kwenye meli, wizi wa mizigo, yakiwamo makontena na vifaa vya magari kama vile taa na redio; uchakachuaji wa mafuta; urasimu na ucheleweshaji wa mizigo kutoka bandarini; ukubwa wa tozo za bandari na barabara; na ugumu wa magari ya mizigo kufika na kutoka bandarini, taratibu za kutoaa mizigo zisizotabirika na rushwa bandarini na barabarani.
Asilimia 90 ya biashara yote ya Tanzania na nchi za nje inapita katika bandari ya Dar es Salaam.

Nchi sita za jirani – Malawi, Zambia, Kongo, Burundi, Rwanda na Uganda ambazo hazina bandari zinaitumia bandari ya Dar es Salaam. Hata hivyo bandari ya Dar es Salaam inakabiriwa na ushindani mkubwa kutoka bandari ya Mombasa inayofanya kazi kwa ufanisi mzuri zaidi. Bandari ya Beira Msumbiji ina ushindani mkubwa kwa mizigo inayoenda Malawi, Zambia na hata Kongo.

Bandari ya Dar es Salaam haifanyi kazi kwa ufanisi. Utafiti wa Benki ya Dunia unaonyesha kuwa, ikiwa bandari ya Dar es Salaam itafanya kazi kwa ufanisi kama bandari ya Mombasa, pato la taifa la Tanzania litaongezeka kwa dola bilioni 1.8 kila mwaka sawa na asilimia 7 ya pato la taifa la sasa. Nchi jirani zinazotumia bandari ya Dar es Salaam zitaongeza mapato yao kwa dola milioni 800. Utendaji mbovu wa bandari zetu unatokana na ombwe la uongozi, ufisadi na menejimenti mbovu.

Tanzania inaweza kukuza uchumi wake kwa asilimia 10 kila mwaka na kuongeza ajira kwa wingi ikiwa itatumia fursa za jiografia zikiwemo bandari zake kuwa kituo cha usafirishaji, viwanda na biashara kwa nchi sita zinazopakana na Tanzania na ambazo hazina bandari.

Serikali inaelewa wazi utendaji wa bandari ya Dar es Salaam ni mbovu na hauridhishi. Hata hivyo, kwa sababu ya ombwe la uongozi, serikali inasuasua kufanya mabadiliko yanayohitajika kuongeza tija na ufanisi wa bandari ya Dar es Salaam.

Uzembe wa utendaji wa bandari ya Dar es Salaam unasababisha msongamano wa meli zenye mizigo ya kushusha bandarini. Ukisafiri kwa ndege kati ya Zanzibar na Dar es Salaam unaweza kuhesabu meli zaidi ya ishirini zilizoweka nanga zikisubiri kupewa ruhusa ya kwenda gatini kushusha mizigo. Katika mwaka 2012 muda wa meli kusubiri kupata gati la kushushia mizigo bandari ya Dar es Salaam ilikuwa siku 10 ukilinganisha na chini ya siku moja bandari ya Mombasa. Hata baada ya makontena kupakuliwa inachukua muda mrefu – wastani wa siku 10 au zaidi kushusha mizigo na kupata kibali cha kuisafirisha toka bandarini.

Ukilinganisha na bandari ya Mombasa gharama za bandari ya Dar es Salaam ni za juu kwa asilimia 22 kwa kila kontena. Gharama za tozo na ushuru mbalimbali za bandari ya Dar es Salaam ni za juu kwa asilimia 74 ukilinganisha na bandari ya Mombasa. Kwa kila dola 100 za gharama ya kushusha mizigo Mombasa, gharama ya kushusha mizigo hiyo hiyo Dar es Salaam ni dola 174. Katika hali hii tusistaajabu nchi jirani kuikimbia bandari ya Dar es Salaam.

Utendaji wa Shirika la Reli umeporomoka sana. Shirika la Reli lilisafirisha mizigo ya tani 154,000 mwaka 2012 ukilinganisha na tani 1,446,000 mwaka 2002. Kuanguka kwa shirika la reli pia kunachangia uharibifu mkubwa wa barabara kwani mizigo mizito inayostahiki kusafirishwa kwa garimoshi inasafirishwa kwa malori yenye uzito zaidi ya viwango vya barabara. Ikiwa reli ya kati itafanya kazi kwa ufanisi na tija ya hali ya juu. Nchi za Kongo, Burundi, Rwanda na Uganda wanaweza kutumia reli ya kati kusafirisha mizigo yao kwenda na kutoka Dar es Salaam.

Reli ya TAZARA haijatumiwa kwa kadri ya uwezo wake. TAZARA ilisafirisha mizigo ya tani 259,000 mwaka 2012 ukilinganisha na tani 677,000 mwaka 2002. Kwa kawaida usafiri wa reli ni wa gharama za chini ukilinganisha na usafiri wa barabara. Tuna wajibu wa kuimarisha utendaji wa Shirika la Reli na TAZARA ili kuongeza ushindani wa kibiashara na kukuza uchumi wetu.

Kuhusu Shirikisho la Kisiasa la Afrika Mashariki Rais alieleza kuwa “Katika Mkutano wa 14 wa Wakuu wa Nchi wanachama uliofanyika tarehe 30 Novemba, 2012, Nairobi, tulipokea taarifa ya hatua iliyofikiwa kuhusu mchakato wa kutaka kuanzishwa kwa Shirikisho. Mkutano huo uliagiza nchi wanachama kujadiliana zaidi kuhusu mpango kazi wa kufikia Shirikisho la Kisiasa na mpango wa kutekeleza mapendekezo mengine yaliyotolewa na Timu ya Wataalamu. Inategemewa kuwa Baraza la Mawaziri litawasilisha mapendekezo ya majadiliano hayo katika Mkutano wa 15 wa Wakuu wa Nchi mwezi Novemba, 2013. Iweje leo wenzetu hawa waamue kuanzisha mchakato wao wa kuharakisha Shirikisho la Afrika Mashariki.”

Rais Museveni amekuwa mstari wa mbele kuharakisha kufikia Shirikisho la Kisiasa. Wachambuzi wa siasa za Uganda wanaamini ana lengo la kuwa Rais wa kwanza wa Shirikisho la Afrika Mashariki. Tanzania imekuwa kikwazo kwani Watanzania wengi wanaamini haraka haraka haina baraka. Wanataka ushirikiano wa Afrika Mashariki ufuate hatua zilizoanishwa katika Mkataba ulioanzisha Jumuiya ambazo ni Umoja wa Forodha, Soko la Pamoja, Umoja wa Sarafu na Fedha, na hatimaye Shirikisho la kisiasa litakalopigiwa kura ya maoni na kila nchi.

Katika suala la soko la pamoja Tanzania imesita kuruhusu masuala ya ardhi, ajira na uhamiaji yaingizwe mara moja katika soko la pamoja la Afrika Mashariki. Nchini Kenya suala la ardhi linaendelea kuleta mvutano mkali. Ni muhimu kwa serikali kuwa makini sana katika sera ya ardhi, wananchi wasiporwe ardhi yao.

Hata hivyo tusiwe na wasiwasi. Shirikisho la Kisiasa la Kenya, Uganda na Rwanda ni ndoto ya mchana. Katika karne ya 21, shirikisho la kisiasa lazima lijikite katika mfumo wa demokrasia. Kenya imepiga hatua kubwa katika ujenzi wa demokrasia lakini bado hawajafanikiwa kujenga umoja wa kitaifa. Baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2007 kulitokea machafuko makubwa. Zaidi ya watu elfu moja walipoteza maisha. Maelfu walikuwa wakimbizi wa ndani. Rais Kikwete na Rais Mstaafu Mkapa walishiriki katika kuwasuluhisha Wakenya na hatimaye kupata serikali ya umoja wa kitaifa. Baada ya uchaguzi wa mwaka huu Uhuru Kenyatta aliibuka kuwa mshindi wa Urais. Mpaka hivi sasa Rais Kenyatta anasuasua kufanya ziara kamili Kenya ya magharibi.

Rwanda na Uganda ni utawala wa kidikteta. Rais Museveni alibadilisha katiba na kuondoa kipengere cha ukomo wa mtu mmoja kuchaguliwa kuwa Rais. Kipindi cha mwisho cha Rais Kagame kinamalizika mwaka 2017 na tayari kuna kauli kuwa wananchi wa Rwanda wanataka aendelee kuwa Rais baada ya 2017.
Kitendo cha kuvunja taratibu na itifaki ya Jumuiya ya Afrika Mashariki kinaonesha wazi kuwa viongozi hawa hawaaminiki. Ikiwa hawakuheshimu makubaliano ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki wanaweza pia baadhi yao wasiheshimu makubaliano baina yao.

CHANGAMOTO KWA TANZANIA
1. Tujenge umoja wa kitaifa wa dhati unaojikita katika kuheshimu hakimu na kujenga misingi imara ya demokrasia. Tuendelee kuhakikisha mchakato wa kupata katiba mpya unakuwa shirikishi.

2. Tuimarishe miundombinu na ushindani wa kiuchumi wa Tanzania

3. Tujenge uchumi unaotumia vizuri raslimali za nchi na ukuaji wa uchumi unaongeza ajira na kuwanufaisha wananchi wote.

5. Tuimarishe vyombo vyetu vya ulinzi na usalama viwe na maadili ya juu na vifanye kazi kwa weledi. Tusipuuze uwezekano wa jirani zetu kula njama kutuhujumu

6. Katika kikao cha Viongozi Wakuu wa Afrika Mashariki, Rais Kikwete awaondolee uvivu wenzake na kuwaeleza bayana mambo wanayofanya hayakubaliki na yanadhoofisha Jumuiya ya Afrika Mashariki


Ibrahim Haruna Lipumba
Mwenyekiti,
Jumapili, 10 Novemba 2013.
Dar Es Salaam.

0 Weka maoni yako hapa:

Post a Comment

COMMENT HAPA