Jul 31, 2014

Dida afunguka, simu ndio chanzo cha kuachana na Ezden, 'alinichapa mikanda', azungumzia mpango wa ndoa nyingine

Dida afunguka,  simu ndio chanzo cha kuachana na Ezden,

Dida Shaibu, mtangazaji wa kipindi cha Mitikisiko ya Pwani amefunguka Exclusively kupitia Sunrise ya 100.5 Times Fm  inayoongozwa na Fadhili Haule na kueleza chanzo cha ndoa yake  na Ezden ‘The Rocker’ Jumanne kuvunjika. Ndoa iliyodumu kwa muda wa mwaka mmoja tu.

Dida ameeleza kuwa mzizi wa tatizo lililopelekea ugomvi mkubwa kati yao ni simu ya mkononi ya mumewe huyo wa wazamani baada ya kutaka kuitumia kucheza game na kugundua kuwa imewekewa password kwa mara ya kwanza katika uhusiano wao.

 “Tatizo kubwa la ugomvi wangu na X-Husband, tatizo kubwa lilikuwa ni simu. Nakumbuka ilikuwa siku ya Jumatano tumetoka kazini. Tukawa tuko kawaida, unajua sisi huwa tunataniana sana. Kwa hiyo aliacha simu yake kitandani, unajua mimi huwa nacheza game kupitia simu yake. Kwa hiyo mimi nikachukua simu yake nikakuta ameweka password kitu ambacho sio cha kawaida. Kwa hiyo mimi ikabidi nimuulize…nikamuita, tulikuwa tunaitana ‘mshikaji wangu mshikaji wangu’. Kwa hiyo alikuwa yuko bafuni anaoga, kwa sababu nyumba ni self-contained, kwa hiyo nikawa namwambia ‘duh mshikaji wangu mbona umeweka password?’ yaani kama utani tu, akaniamba ‘aah we iache simu yangu’.” Dida ameiambia Sunrise ya Times Fm.

 
Wanandoa washikaji, Dida na Ezden (December, 2013)


Amesema Ezden alishikilia msimamo wake kutomuonesha password kitu ambacho kilimpa hisia na wasiwasi kuwa huenda jamaa anamsaliti (anamichepuko) ameficha kupitia simu hiyo na kuanza kuongeza nguvu ya kuomba apewe password ili aondoe wasiwawasi wake lakini hakufaulu zoezi hilo.

Ameiambia Sunrise ya 100.5 Times Fm kuwa kitu kilichomfanya afikirie kuwa ameonewa kwa kunyimwa password ni uhuru aliokuwa nao mumewe huyo wa zamani kupitia application za kidijitali.

Amesema Ezden alikuwa na uwezo wa kuona kila kinachofanyika kwenye simu ya Dida hata  kupata jumbe zinazoenda kwenye simu ya Dida kabla mwenyewe hajazipata.


Dida na Ezden wakifunga ndoa July,2013

“Simu yangu anauwezo wa kushika akakaa nayo, simu yangu anaweza kushika akadownload vitu vya kuweza kufatilia Dida anaenda wapi, Dida anafanya nini. Messages zangu za WhatsApp alikuwa anaweza kupata yeye kabla yangu mimi. Na kingine kikubwa ni kwamba alikuwa anaweza kudownload maongezi ambayo naongea na watu. Lakini hajawahi kukuta maongezi mabaya na watu….Nikiwa Kawe simu yake inamuonesha kuwa Dida yuko Kawe.” Ameeleza.

Hata hivyo, ametaja kuwa wasiwasi wa mumewe huyo wa zamani na mabadiliko yake katika matumizi ya simu yalitokana na ujumbe ambao alikuwa ametumiwa na mwanaume ambaye kwake yeye ni mteja.
Lakini ujumbe huo haukueleweka vizuri kwa sababu kuna kitu anadhani kilimiss kwenye ujumbe huo kilichosababisha ieleweke tofauti (Kama mtu anaechepuka nae).

Ameeleza kuwa alipoendelea kuomba zaidi password na hali ya kutoelewana kuongezeka akajikuta akipigwa vibao na hapo mambo yakazidi kuwa mabaya kwenye uhusiano huo.

“Alinipiga kibao, sio kibao tu, Vibao vya uhakika….baada ya kupigwa mimi nilishikwa na hasira kwa sababu alinipiga na baadae akaona kibao hakitoshi. Akachukua mkanda, mkanda huu wenu wa suruali lakini ulikuwa mzito akawa ananichapa nao ‘kwa nini unataka kupishika vitu vyangu’.

Anasema kutokana na kipigo hicho aliumia kichwani na kuelekea hospitali, lakini aliporudi nyumbani alikuta mwenzake ameshachukua vitu vyote alivyokuwa anavimiliki (alivyoenda navyo).
Alipoulizwa nani alimuacha mwenzake:

“Sitaki kusema nani kamuacha mwenzake kwa sababu mimi ndiye niliomba divorce. Katika maisha ya mwanadamu wanasema mwanamke hauwezi kumuacha mwanaume ila mwanaume anaweza kumuacha mwanamke. Lakini mimi nahisi kama tumeachana.”

Katika hatua nyingine, Dida aliulizwa kuhusu mpango wake wa baadae katika uhusiano wake kama ana mpango wa kuolewa tena.  Alisema hana mpango huo kwa sasa.

“Kwa sasa sina mpango wowote wa kuhusiana na suala la ndoa. Yaani sina na sitegemei. Na kama kuna mtu anafikiria kwa sababu napata maombi mengi sana. Washindwe na walegee. Kwamba labda naweza kusema mwenyezi Mungu amenijalia kuwa nabahati hiyo…Sio kupendwa yaani tuseme, unajua binadamu anakupenda mwingine anakujaribu. Sasa hivi watanifuata wanaume wengi sana kila mmoja atakuja kwa sampuli anayoijua yeye. Huyu atajifanya yeye ndiye ana mahaba kuliko Yule. Mwingine anasema ‘atapigaje mwanamke?’ kumbe yeye ndiye mdundaje kwelikweli kuliko hata yule.

“Sitaki kuja kujutia maisha yangu, sitaki kuja kujutia maamuzi yangu. Huwa nafanya kitu kwa kuangalia mbele zaidi. Mimi nina biashara zangu, nina maisha yangu. Namshukuru Mungu amenijalia mtoto mmoja. Kwa hiyo nahitaji mtoto wangu awe na maadili fulani hivi ambayo ya kusema kwamba huyu ni mama..nahitaji kumsomesha, nahitaji awe hivi. Lakini sitaki mwanangu apate matatizo haya ambayo labda mama yake nimepitia. Lakini hii yote nasema ni ujasiri. Nasema Mwenyezi Mungu labda ananionesha njia.”

0 Weka maoni yako hapa:

Post a Comment

COMMENT HAPA