Apr 2, 2012

WABUNGE CHADEMA WAPIGWA MAPANGA

WABUNGE wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Mkoani Mwanza, Highness Kiwia (Ilemela), na Salvatori Machemli (Ukerewe), wamenusurika kuuawa baada ya kuvamiwa na watu wanaosadikiwa kuwa ni wafuasi wa CCM kisha kukatwa
Salvatory Machemli
mapanga sehemu mbali mbali za miili yao, ambapo Mbunge Kiwia inadaiwa hali yake ni mbaya sana.
Mbali na wabunge hao kujeruhiwa vibaya, pia mbunge wa Jimbo la Nyamagana jijini hapa, Ezekiel Wenje (Chadema), naye inadaiwa amenusurika kipigo pamoja na kukatwa mapanga na wafuasi hao wa CCM, huku wafuasi wengine watano wa Chadema wakijeruhiwa vibaya katika tukio hilo la aina yake ambalo limelaaniwa vikali na wananchi wa mkoa wa Mwanza na taifa kwa ujumla.
Tukio hilo limetokea majira ya saa 7 usiku wa kuamkia leo, ambapo wabunge hao wakidaiwa walikuwa wakiwasambaza mawakala wa chama chao kwenda majumbani kwa ajili ya kujiandaa kwenda kusimamia kura za mgombea wa Chadema Kata ya Kirumba, Dany Kahungu katika uchaguzi mdogo uliofanyika jana.
Taarifa zaidi zinadai kwamba, wabunge hao walikutwa na wafuasi wa CCM wakiwa wanatoa rushwa nyumba kwa nyumba, katika eneo la Ibanda Kabuholo kata hiyo ya Kirumba ambapo, jambo ambalo Jeshi la Polisi limeshindwa kuthibitisha juu ya madai ya utoaji huo wa rushwa.
Kwa mujibu wa taarifa hizo ambazo mwandishi wa habari hizi alizipata wa kuamkia jana, Mbunge wa Ilemela, Kiwia ndiye aliyeumizwa zaidi kutokana na kupata majeraha makubwa sehemu za kichwani, mgongoni pamoja na maeneo ya makalio, ambapo alikimbizwa katika Hospitali ya Rufaa ya Bugando (BMC), ya jijini Mwanza kwa matibabu zaidi.
Wakati Mbunge Kiwia akidaiwa kuumizwa vibaya na wafuasi hao wa CCM, taarifa zingine zinasema Mbunge wa Ukerewe, Machemli yeye alikatwa mapanga sehemu mbali mbali za mwili wake, lakini hajaumia sana.
Highness Kiwia
Uongozi wa Hospitali ya Bugando umethibitisha kufikishwa na kupatiwa matibabu kwa wabunge hao pamoja na baadhi ya wafuasi wa Chadema katika hospitali hiyo, na kwamba Mbunge wa Ilemela aliondolewa haraka hospitalini hapo kwa ajili ya kupelekwa sehemu nyingine kwa matibabu zaidi.
“Kweli Mbunge wa Ilemela na yule wa Ukerewe waliletwa hapa Bugando wakiwa wamejeruhiwa vibaya sana. Lakini baada ya kupatiwa matibabu, huyo mbunge Kiwia aliondolewa haraka sana na wenzake hospitalini hapa. Hatujui walimpeleka wapi maana hiyo sasa ni mambo binafsi.
“Inawezekana huyu mbunge wa Ilemela amesafirishwa kwenda Dar es Salaam au KCMC. Lakini ni vizuri ukawasiliana na Muuguzi wa zamu ili upate ufafanuzi zaidi”, alisema Ofisa Tawala wa Hospitali ya Bugando, Joackim Wangabo.
Jitihada za kumpata muuguzi wa zamu ziligonga mwamba, baada ya kuelezwa kwamba yupo sehemu nyeti akitoa huduma kwa wagonjwa wengine. Lakini Daktari mmoja aliyekutwa mapokezi hospitalini hapo ambaye alikataa kutaja jina lake alipoulizwa alikiri kumpokea Mbunge Kiwia na watu wengine wawili akiwa amejeruhiwa vibaya kwa mapanga, na kwamba alishaondolewa hospitalini hapo na hajui kapelekwa wapi.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Liberatus Barlow (RPC), aliwaambia waandishi wa habari leo kwamba: “Ni kweli wabunge hao wamevamiwa na kujeruhiwa kwa mapanga usiku, na sisi leo (jana), majira ya saa 7:20 tulipokea taarifa kuwa wafuasi wa CCM wamewateka na kuwaweka chini ya ulinzi wabunge watatu wa Chadema”.
Alisema baada ya kupata taarifa hizo, muda mfupi polisi walifanikiwa kufika eneo la tukio na kuwakuta wabunge hao ambao ni Kiwia, Wenje na Machemri wakiwa wamewekwa chini ya ulinzi na wafuasi hao wa CCM, ambapo polisi walipambana na kufanikiwa kuwaokoa.
“Mbunge Kiwia alikuwa amejeruhiwa kichwani na kukimbizwa katika hospitali ya Rufaa ya Bugango kwa ajili ya matibabu. Majeruhi wengine ni pamoja na dereva wa mbunge wa Ukerewe jina hatujalipata yeye amejeruhiwa mguu wa kushoto, na Ahmed Waziri ambaye amekatwa sehemu ya kiganja mkono wa kulia”, alifafanua RPC Barlow.
Kamanda Barlow aliwataja majeruhi wengine watatu waliokimbizwa katika hospitali ya mkoa ya Sekou Toure na kulazwa kuwa ni pamoja na Haji Mkwenda (21), ambaye amevunjika mguu wa kulia, Judith Madaru (26), ambaye amechomwa kisu sehemu ya ziwa upande wa kushoto na Ivori Festo Machimba (26), ambaye amejeruhiwa kichwani na mdomoni.
Barlow alifafanua kuwa walipofika katika eneo la tukio polisi walikuta magari matatu huku mawili yakiwa na funguo na kuyaokoa kwa kuyaondoa, baada ya wananchi kuanza kuyarushia mawe huku gari moja ambalo halikuwa na funguo liliondolewa eneo hilo kwa kuvutwa na gari la kuvutia magari.
Alitaja namba za magari yaliyokutwa kwenye eneo la tukio kuwa ni pamoja na T 377 ARF linalomilikiwa na mbunge Kiwia, T 729 DAD linalomilikiwa na Mohamed Juma pamoja na T 397 ANU aina ya Land Cruiser ambalo mmiliki wake hakupatikana.
Wabunge hao simu zao zote zilikuwa zimezimwa hadi tunakwenda mitamboni.
Baadhi ya wananchi wakiwemo wanaharakati na wachambuzi wa mambo ya kisiasa mkoani Mwanza, wamelaani vikali unyama huo uliofanywa na wafuasi wa CCM, na kusema kamwe chama hicho tawala hakitapoteza muda kuondoka madarakani.
“Tunalaani vikali sana unyama huu waliofanyiwa wabunge wetu hawa. Hizi ni siasa chafu zilizoanza kutumiwa na CCM, na kamwe siku za mwisho za utawala wa chama hiki tawala umefika.
“Tunaliomba jeshi la polisi lihakikishe linawakamata na kuwafikisha mahakamani watu wote waliohusika katika tukio hilo bila kuangalia wanatoka chama gani na ni akina nani. Uonevu huu hauvumili, tunataka kuona hatua kali zinachukuliwa”, alisema mkazi mmoja wa jiji la Mwanza, Neema Marco.

Imeandaliwa na Sitta Tuma, Mwanza 
kwa msaada wa fikira pevu

Wakati huo huo, Mbunge wa Ubungo, John Mnyika ametoa taarifa kulaani tukio hoilo.

0 Weka maoni yako hapa:

Post a Comment

COMMENT HAPA