Jun 28, 2013

VIONGOZI WA CUF TAIFA WATEKWA MTWARA

MH: PROFESA LIPUMBA
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
 
TAREHE 28/06/2012

KUTEKWA KWA NAIBU MKURUGENZI WA OGANAIZESHENI UCHAGUZI NA BUNGE WA CHAMA CHA WANANCHI CUF TAIFA MHE. SHAWEJI MKETO NA VIONGOZI WENGINE WA CUF MKOANI MTWARA.

Juzi Jumatano tarehe 26 Juni 2013 Mkurugenzi wetu wa Oganaizesheni Uchaguzi na Bunge mhe. Shaweji Mketo alitumwa na chama chetu kuhudhuria kesi inayowakabili viongozi mbalimbali wa CUF katika mahakama ya Mtwara Mjini (Kesi inayomkabili MHE.KATANI AHMAD KATANI na wenzake).

Mhe. Mketo alipotoka mahakamani alifanya kikao na wanachama wa CUF Mtwara mjini ambao walimueleza unyanyasaji na ukatili mkubwa ambao wanajeshi na polisi wanawafanyia wananchi wa Mtwara. Palitolewa ushahidi wa binti mmoja aliyenajisiwa na binti huyo aliripoti tukio husika katika kituo cha polisi cha Msimbati kilichoko Mtwara na binti huyo alipeleka polisi hadi ushahidi wa wa mipira ya kiume iliyotumika kumfanyia unyama huo lakini polisi hawakuchukua hatua yoyote hadi leo.

Mhe. Mketo na viongozi wengine waandamizi watano walielekea maeneo ya kijiji cha Msimbati ambako binti huyo amesitiriwa baada ya unyama huo. Mzazi wa binti aliyebakwa anajulikana kwa jina la SELEMANI BIN OMARI. Mhe. Mketo na viongozi aliokuwa nao walifika kijiji cha Msimbati na kukusanya ushahidi walioufuata na kisha wakakutana na wakakutana na mwenyekiti wa kijiji cha Msimbati ambaye anatoka Chama Cha Wananchi CUF wakafanya naye kikao kifupi na kisha wakaondoka kurejea Mtwara Mjini.

Kati ya saa 11.30 – 12.00 jioni walifika eneo la kilometa tatu kabla ya kuingia mjini(Eneo la njia pacha). Magari mawili ya kijeshi moja likiwa aina ya TATA na lingine likiwa DEFENDER ya jeshi yaliziba barabara. Ilibidi gari ya mhe. Mketo iliyokuwa ikipeperusha bendera ya chama chetu isimame(Gari hii ni aina ya NISSAN PATROL yenye namba T 866 BGW – Mali ya Chama Cha Wananchi CUF). Askari jeshi zaidi ya 50 waliivamia gari yetu na kuanza kuwapiga mhe. Mketo na wenzie bila kuwajulisha chochote na kisha kuwatupa katika karandinga la jeshi kama vile wanatupa mizigo.

Baada ya kuwateka waliwapeleka katika kambi ya jeshi ya NALIENDERO iliyoko maeneo ya jirani na Mtwara mjini na kuwashikilia huko tangu jana jioni hadi leo mchana.

Mimi binafsi nilifikishiwa taarifa hizo na Mhe. Mtatiro majira ya saa 2 usiku na nilipopewa taarifa hizo nilipiga simu za mhe. Mketo (Naibu Mkurugenzi wa Oganaizesheni Uchaguzi na Bunge CUF taifa) na Mhe. Kulaga(Katibu wa Wilaya) na namba zao zilikuwa zinapokelewa na wanajeshi hao huku wakijibu matusi. Taarifa tulizonazo ni kuwa Mh. Mketo na wenzie wanateswa na ndiyo maana simu zao zikipigwa wanajeshi hao watesaji wanajibu matusi.

Mhe. Mtatiro alimpigia RPC wa Mtwara na RPC akajibu kuwa yeye hana taarifa na viongozi wetu kushikiliwa na hajui wako wapi. Tumeendelea kuwajulisha viongozi mbalimbali wa jeshi la polisi na ulinzi juu ya tukio hili. Hivyo, pamoja na mashuhuda kuona wakipelekwa katika kambi hiyo ya jeshi bado kama chama hatujui hasa wako wapi kwani simu zao zinapokelewa na watekaji na watesaji wao tu.

CUF – Chama Cha Wananchi kimesikitishwa na kufadhaishwa na kitendo hiki cha utekaji nyara viongozi na raia wasio na hatia yoyote. Tumeumizwa zaidi kaa chama baada ya kuona kuwa jeshi la Ulinzi la Tanzania lenye mamlaka ya kulinda mipaka ya nchi hivi sasa limeachiwa sasa kazi ya polisi ya kukamata raia. Pamoja na Jeshi kuachiwa kazi za polisi(JAMBO AMBALO NI KINYUME NA SHERIA), wanajeshi hao wanatumia mamlaka hayo batili kuteka wananchi, kuwapeleka kwenye kambi za jeshi na kuwateka kwa siku watakazotaka. Nchi yetu inaelekea wapi? Leo Tanzania mwananchi anakamatwa na askari Jeshi badala ya polisi! Haya mamlaka askari jeshi wamepewa na nani na wameyatoa wapi?

Kwa mujibu wa sheria hata ikitokea mazingira ambayo hayakwepeki kwa askari wa jeshi au vikosi vingine kumkamata raia, ni sharti la kwanza kuwa lazima wamkamate raia huyo bila nguvu na wamkabidhi raia huyo kwa jeshi la polisi mara moja. Sasa iweje Mketo na wenzie wakamatwe na wanajeshi (kinyume na sheria na bila kufanya kosa lolote) saa 11 jioni eneo ambalo ni kilometa tatu tu kutoka kituo kikuu cha polisi Mtwara mjini na badala yake wanapelekwa kwenye kambi ya jeshi kuhojiwa kuteswa na kushikiliwa? Leo jeshi la ulinzi ndiyo lina kazi ya kuhoji raia?

Tunataka serikali na jeshi viwajibike haraka iwezeikanavyo. Jeshi la Ulinzi liache mara moja vitendo vya kinyama vya kuteka na kutesa wananchi wa Mtwara na viongozi wa CUF na tunataka wanajeshi wamuachie mhe. Mketo na viongozi wetu mara moja na bila masharti yoyote.

Tayari tumewasiliana na wanasheria wetu tokea jana usiku na timu yetu ya mawakili iko Mtwara Mjini tangu asubuhi hii kufuatilia suala hili na kuhakikisha kuwa viongozi wetu wanapata haki. 
Tunaitaka serikali isiendeleze vitendo vya namna hii kwani vinawavunja moyo wananchi na vinawakatisha tamaa na hali hii ikiendelea wananchi watavichukia vyombo vya ulinzi na usalama, jambo ambalo litakuwa na mustakabali mbaya.

Tunalitaka pia jeshi la polisi lifanyie kazi ukatili aliotendewa binti ya Selemani Omari kwa kubakwa na askari jeshi na askari husika afuatiliwe na sheria za nchi zichukue mkondo wake. Sambamba na hilo ,asasi za kiraia, za kisheria na za kutetea haki za wanawake zifanye juhudi kubwa kuhakikisha kuwa wanafika Msimbati na kukutana na binti huyu aliyebakwa ili asaidiwe kisaikolojia kwani kitendo alichofanyiwa ni kovu la kudumu kwa maisha yake. Chama Cha Wananchi CUF kinatoa pole kwa binti aliyebakwa na familia yake, wawe watulivu na wasaidiane na kila mdai haki kupigania haki yao.

Aidha tunatoa wito kwa vyombo vya habari vifanye juhudi kubwa kuweka kambi Mtwara ili kujionea ukatili wanaofanyiwa wananchi na kuuripoti kwa watanzania wote, wananchi wa Mtwara wasitengwe na asasi zinazoweza kutangaza ukatili wanaofanyiwa.

Imetolewa na :-
Prof. Ibrahim Lipumba
Mwenyekiti wa CUF-Chama cha wanachi, taifa
Mh.Prof.Ibrahim Lipumba

0 Weka maoni yako hapa:

Post a Comment

COMMENT HAPA