Jun 29, 2013

Barthez achana mkataba wa Kaseja Yanga

 
 JUMA KASEJA

VIGOGO wa Yanga walikuwa wanabishana kuhusu nani wamsainishe kati ya kipa Deo Munishi ‘Dida’ na Juma Kaseja, wakashindwa kufikia muafaka. Ngoma ikalala.
Wakaamka asubuhi, wakakaa tena, wakafikiria weee, hawakufikia muafaka, baadaye wakapata jibu. Wakamkabidhi kipa wao namba moja, Ally Mustapha ‘Barthez’ rungu afanye uamuzi kati ya Kaseja na Dida nani anataka afanye naye kazi Jangwani.
Unajua alichofanya Barthez akawaambia: “Nileteeni Dida.” Mwenyekiti wa Usajili wa Yanga, Abdallah Bin Kleb akampigia simu Dida akakutana naye chemba juzi Alhamisi jioni jijini Dar es Salaam na bila ajizi akamsainisha mkataba wa miaka miwili, biashara ikawa imeisha.
Kwa maana hiyo mkataba wa Kaseja ukawa kama umechanwa Jangwani, lakini mkataba wa Dida ukapigwa muhuri, sahihi na dole gumba kijana akale chake akaondoka.
Simba imetangaza kumtema Kaseja na kwa sasa anahaha kusaka klabu mpya.
Bin Kleb aliliambia Mwanaspoti kuwa walifikiria kwanza kumsajili Kaseja wakakutana na kukuna vichwa sana kabla ya kuamua kuachana na kipa huyo ambaye ni nahodha wa  Taifa Stars baada ya kupata pia uamuzi wa Barthez.
“Tulianza kukusanya maoni kuhusiana na suala la kipa, kuna wadau wa Yanga walisema tunaweza kumsajili Kaseja huku wengine wakisema tuachane naye kwani aliwahi kudumu Yanga kwa msimu mmoja tu pamoja na kusajiliwa kwa pesa nyingi,” alisema Bin Kleb.
“Kwa kifupi Barthez ndiye aliyepiga kura ya veto kwa Dida na kusisitiza kuwa lazima asajiliwe kipa huyo ambaye aliwahi kusota naye benchi katika klabu ya Simba huku Kaseja akitawala. Hakukuwa na pingamizi zaidi ya kuanza mazungumzo naye Dida,” alisema.
Bin Kleb alisema pamoja na Dida kukumbwa na kashfa ya rushwa iliyohusisha klabu ya Simba, msukumo mwingine walioupata ni uamuzi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) ambayo ilimsafisha kipa huyo na wenzake watatu.
“Naomba wana Yanga wampe sapoti kubwa kama wachezaji wengine, ambao waliwahi kuichezea Simba kwa kipindi fulani,” alisema kiongozi huyo huku Dida akiomba sapoti ya wachezaji wenzake.
“Naomba mniamini kama ilivyokuwa kwa Kaseja ambaye alicheza Yanga huku akiwa ametokea Simba ambako alikuwa amecheza zaidi ya miaka saba. Naomba wanachama, wazee wa Yanga, wadau, mashabiki waniamini kama  ulivyofanya uongozi nitafanya kazi nzuri.”
Dida, Barthez na Kaseja wote wamekuwa kucheza pamoja Simba.

chanzo  http://www.mwanaspoti.co.tz

0 Weka maoni yako hapa:

Post a Comment

COMMENT HAPA