KUFUATIA KATIBA YA NZANZIBAR KUKINZANA NA KATIBA YA JAMHURI HII NDIO TAARIFA KUTOKA CUF KUHUSU MCHAKATO WA KATIBA MPYA
PROFESA IBRAHIMU HARUNA LIPUMBA
THE CIVIC UNITED FRONT - CUF,
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI.
Imetolewa na Mwenyekiti wa CUF - Taifa, Prof. Ibrahim Haruna Lipumba.
Tanzania iko mbioni kukabiliwa na mgogoro mkubwa wa kikatiba. Tayari
mabadiliko ya katiba ya Zanzibar yanakinzana na Katiba ya Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania ya 1977 lakini hayakinzani na sheria mama ambayo ni
makubaliano ya Muungano (Articles of the Union).
Ili
kukabiliana na changamoto ya kupata katiba mpya, kuwa na daftari safi la
wapiga kura, kuunda Tume huru ya uchaguzi, na kuwa na uchaguzi ulio
huru na wa haki 2015, Rais Kikwete baada ya kushauriana na wadau
mbalimbali aunde serikali ya umoja wa kitaifa.
Serikali ya
Umoja wa Kitaifa pia iimarishe uwajibikaji wa vyombo vya dola na
viongozi, ishughulikie kadhia ya matumizi mabaya ya fedha za umma na
iimarishe ukusanyaji wa mapato serikali ili miradi ya maendeleo kama
vile ujenzi wa barabara na ufuaji wa umeme iweze kukamilishwa.
Mchakato wa Katiba mpya unapaswa kuwapa wananchi matumaini ya kujenga
Tanzania mpya yenye haki sawa kwa wote na itakayojenga uchumi ambao
hatua kwa hatua, utaleta neema kwa wananchi wote. Katiba itamke wazi
rasilimali na maliasili ya nchi itatumiwa kwa manufaa ya wananchi wote
na vizazi vijavyo. Uandikaji wa katiba mpya ni fursa adhimu ya kujenga
muafaka wa kitaifa unaowapa imani na matumaini wananchi kuwa mfumo wa
utawala, siasa na uchumi unaowekwa na katiba unalinda maslahi yao na
utawaletea maendeleo wayatakayo.
Mchakato wa kupata katiba mpya
kabla ya 2015 una vikwazo vingi. Ni wazi Katiba Mpya haiwezi kapatikani
ifikapo tarehe 26 Aprili 2014 wakati tunasheherekea miaka 50 ya
Muungano. Rasimu ya mwisho ya Tume ya Katiba itapatikana mwezi huu. Rais
anawajibika kukamilisha uundaji wa Bunge la Katiba kwa kuteua wabunge
201 baada ya kupata mapendekezo toka wadau mbali mbali vikiwemo vyama
vya siasa, vyama vya wafanyakazi, vyama vya wakulima, taasisi za dini na
kadhalika. Itakuwa bahati kama Bunge la katiba litaweza kuanza shughuli
zake katika ya kumi la mwisho la mwezi wa Januari.
Tume ya
Jaji Warioba imefanya kazi kubwa ya kuratibu maoni na kuja na
mapendekezo ya katiba mpya ambayo hayakushinikizwa na matakwa ya Chama
tawala cha CCM. Mwanazuoni na mchambuzi wa mambo ya katiba na sheria
Prof. Chris Maina Peter amediriki kuita Rasimu ya Katiba kuwa Mapinduzi
ya kimya kimya. Tume imeonyesha ujasiri mkubwa na uhuru wake hasa
ukizingatia pendekezo kuu la Rasimu ya Katiba ni mfumo wa serikali tatu
(Sura ya sita ibara ya 57 – 66) ambao unakinzana na msimamo rasmi wa
Chama tawala cha CCM na wosia wa hayati Mwalimu Nyerere kuhusu mfumo wa
Muungano.
Rasimu ya Katiba ina mabadiliko makubwa ya msingi
ikiwa ni pamoja na mfumo wa Muungano wa serikali tatu, kupunguza mambo
ya muungano kutoka 22 na kuwa saba, kuruhusiwa mgombea binafsi, Rais
kutangazwa kushinda akipata zaidi ya asilimia 50 ya kura zote
zilizopigwa la sivyo uchaguzi urudiwe kwa wale wawili walio ongoza kwa
kura, haki ya wananchi kumuondoa Mbunge wao madarakani, Ukomo wa vipindi
vitatu vya mtu mmoja kuwa mbunge, Tume huru ya uchaguzi, Mawaziri
kutokuwa wabunge, Spika kutokuwa mbunge, haki za watu wenye ulemavu,
kupanuliwa kwa haki za binadamu, kuondolewa kwa viti maalum vya wanawake
na badala yake kila jimbo kuwa na mbunge mwanamke na mbunge mwanaume,
Kuanzishwa kwa Mahakama ya Juu (Supreme Court), haki ya kumiliki mali
na hifadhi ya mali haitahusu mali iliyothibitishwa kwamba haikupatikana
kwa njia halali na mengine mengi.
Hata hivyo mambo mengi muhimu
kama vile umilikaji wa ardhi, maliasili na rasilimali za nchi kutumiwa
kwa manufaa ya wananchi wote, elimu, afya, mazingira ya kukuza uchumi
unaoleta neema kwa wananchi wote, wajibu, uwezo na uhuru wa serikali za
mitaa hayajaingizwa ndani ya katiba kikamilifu kwani rasimu ya katiba
imeshughulikia mambo ya muungano. Hoja ya Tume ya Jaji Warioba ni kuwa
mambo haya yataingizwa kikamilifu katika katiba ya washiriki wa Muungano
– Tanzania Bara na Zanzibar.
Bila kuwepo kwa rasimu ya katiba
ya Tanzani Bara na Marekebisho ya katiba ya Zanzibar isikinzane na
Katiba ya Muungano, zoezi la kupata dira na mwongozo wa kusimamia
utawala, uchumi na siasa za Watanzania haujakamilika. Walau Zanzibar
wana katiba lakini Tanganyika haina katiba wala mchakato wa kuipata
katiba hiyo haujaanza.
Isitoshe rasimu ya Katiba ya Muungano
ina mapungufu makubwa na kuna mambo mengi kama vile mfumo wa Muungano,
Mambo ya Muungano, Ukuu wa Katiba ya Muungano, Mapato ya kugharamia
Muungano yanahitaji mjadala wa kina ili kufikia Muafaka.
Bunge
la Katiba litakuwa na kazi kubwa ya kupata muafaka kuhusu mambo haya
muhimu. Hata wakifikia muafaka na kupata katiba mpya, mapendekezo
yaliyomo katika Rasimu ya Katiba yatahitaji mabadiliko makubwa ya
kisheria na kitaasisi ili kuweza kuitekeleza katiba mpya. Kenya
ilikamilisha katiba yake na kuipitisha kwenye kura ya maoni Agosti 2010.
“Hata hivyo, mabadiliko mbali mbali ya kisheria na kitaasisi kwa ajili
ya utekelezaji wa Katiba hiyo yalichukua zaidi ya miaka miwili na nusu
hadi Uchaguzi Mkuu wa mwezi Machi, 2013.”
Wengi wetu tungependa
zoezi la kupata katiba mpya likamilike kabla ya uchaguzi mkuu wa 2015.
Hali halisi ni wazi zoezi hilo haliwezi kukamilika kwa ufanisi kabla ya
2015. Sheria ya mabadiliko ya katiba inaeleza kuwa ikiwa katiba mpya
haikupitishwa kwenye kura ya maoni, katiba ya sasa itaendelea kutumika.
Mchakato wa kupata katiba mpya, maoni yaliyotolewa na wananchi na
rasimu ya katiba inayotokana na maoni hayo imebainisha wazi Watanzania
hawaitaki katiba ya sasa. Kufanya uchaguzi kwa kutumia katiba ya sasa na
Tume ya Uchaguzi iliyopo hakutakubalika na wananchi na kunaweza kuwa
chanzo cha mgogoro mkubwa wa kisiasa.
Kura ya maoni inakabiliwa na
kikwazo kikubwa cha kutokuwepo kwa daftari la kudumu la wapiga kura
lililoandikisha wapiga kura wote. Daftari la wapiga kura halijaboreshwa
na kuandikisha wapiga kura wapya baada ya uchaguzi mkuu wa 2010.
Mwezi Februari Rais Kikwete alitangaza kuwa vitambulisho vya kitaifa
ambavyo vinatumia alama ya mwili ndivyo vitakavyotumiwa kwa kupigia kura
ya maoni na uchaguzi mkuu. Alieleza mamlaka ya vitambulisho vya taifa
itashirikiana na Tume ya Uchaguzi katika utoaji wa vitambulisho vya
kitaifa ambavyo pia vitakuwa vitambulisho vya kupigia kura.
Zoezi la kuwapa wananchi vitambulisho vya kitaifa linaenda taratibu
sana. NIDA haijakamilisha kutoa vitambulisho hivyo hata kwa wilaya za
Dar es Salaam. Kwa kasi hii ya uandikishaji na utoaji wa vitambulisho
vya kitaifa, zoezi hili halitakamilika katika miaka miwili inayokuja.
Itafika 2015 na wananchi wengi wenye umri wa miaka 18 watakuwa
hawajapata vitambulisho vya taifa.
Vitambulisho vya NEC
havikidhi mahitaji. Vitambulisho hivyo vinaghushiwa kwa urahisi sana.
Wadau wengi hawana imani na daftari la NEC. Ni vyema vitambulisho vya
NIDA vyenye alama za mwili ndivyo vitumiwe kama vitambulisho vya kupigia
kura.
Kura ya maoni kuhusu katiba haiwezi kuendeshwa kwa
ufanisi bila kuwa na daftari la wapiga kura linaloaminika. Kura ya maoni
inabidi ipigwe na wananchi wa pande mbili za Muungano. Tume ya Uchaguzi
ya Taifa inatumia Tume ya Zanzibar kuwa wakala na daftari la ZEC
kubaini wapiga kura wa Zanzibar. Daftari la ZEC linawanyima wananchi
wengi wa Zanzibar kuandikishwa kupiga kura kwa madai kuwa hawana
vitambulisho vya ukaazi.
Tume ya Taifa itawajibika kuwaandikisha Wazanzibari hawa wapate haki ya kupiga kura ya maoni kuhusu katiba.
Ili kusimamia vizuri mchakato wa kupata katiba mpya na kuhakikisha
kuwepo kwa maridhiano na mshikamano wa kitaifa katika kipindi hiki nyeti
ninamshauri Rais Kikwete aunde serikali ya umoja wa kitaifa.
Jukumu kubwa la serikali hiyo iwe kukamilisha mchakato wa kupata katiba
mpya, kuunda Tume Huru ya Uchaguzi, kuandikisha wananchi wote
wanaostahili kupiga kura wapewe vitambulisho vinavyotumia alama ya mwili
ili kuhakikisha uchaguzi wa 2015 unakuwa huru na wa haki.
Serikali ya umoja wa kitaifa pia iimarishe utendaji wa serikali,
ipambane na ubadhirifu ulioainishwa na Mdhibiti na Mkaguzi wa Hesabu za
Serikali na Kamati za Bunge, ianzae kujenga utamaduni wa uwajibikaji na
kutumia vizuri fedha za umma kwa maendeleo ya wananchi.
Ibrahim Haruna Lipumba
Mwenyekiti,
Jumapili, 15 Disemba 2013.
0 Weka maoni yako hapa:
Post a Comment
COMMENT HAPA