Dr. Kitila Mkumbo( Mjumbe kamati kuu chadema) atoa Tamko 
Kufuatia
 taarifa zinazosambazwa kwenye mitandao ya kijamii kuhusu kuhongwa kwa 
Zitto naye kuhonga watu wengine, nikiwemo mimi, ili kutoa siri za chama 
chetu (CHADEMA) kwa lengo ya kukivuraga watu, wengi sana wameniandikia 
email, sms na hapa fb ili nitoe ufafanuzi kuhusu ukweli wa mimi kuhongwa
 na Zitto na mahusiano yangu na mwanasiasa huyu nguli. Mwanzoni 
nilipuuzia na sikutaka kabisa nitoe maoni kuhusu jambo hili kutokana na 
kiwango cha ujinga kilichomo ndani ya waraka huo unaosambazwa. Hata 
hivyo kwa kuwa watu wengi wamenitaka nitoe ufafanuzi, napenda kueleza 
haya yafuatayo:
i)
 Mimi Kitila Mkumbo, pamoja na umaskini wangu, sijawahi kuhongwa popote 
na sitarajii kuhongwa. Taarifa zinazosambazwa juu yangu ni za uwongo wa 
kijinga na uzushi wa kitoto kwa malengo ya siasa nyepesi. Ni wazi kwamba
 wanaosambaza habari chafu juu yangu hawanijui na ndiyo maana wanaweza 
kudiriki kuzusha kwamba mie Kitila Mkumbo naweza kuhongwa sh. 200,000/=.
 Hakuna namna nyingine ya kuthibitisha kwamba waraka huu na maudhui yake
 ni mambo ya kutunga zaidi ya hilo la kuzusha kwamba nami ni miongoni 
mwa watu waliohongwa. 
ii)
 Kuhusu mahusiano yangu na Zitto ni kwamba kijana huyu ni rafiki yangu 
wa miaka mingi tuliyejuana na kuanza urafiki kabla ya hata mie kuijua 
CHADEMA. Urafiki wetu ulikuwepo, upo na utaendelea kuwepo ndani na/au 
nje ya siasa. Wasiopenda hili poleni sana. Mie ni mtu mzima na hakuna 
mtu yeyote mwenye uwezo wa kunichagulia marafiki na/au maadui. 
iii)
 Wanaosambaza waraka huu ni watu woga wa demokrasia na wasioijua 
CHADEMA. Chama hiki kimejipambanua kwa miaka mingi kwamba ni chama 
kinachopigania demokrasia ndani na nje ya chama. Matatizo yetu 
hushughulikiwa kikamilifu ndani ya vikao ambapo huwa tunajadili mambo 
kwa upana. Watu wenye makosa husutwa, huonywa na ikibidi huadhibiwa. 
Kama kweli haya yanayosambazwa yangekuwa na hata chembe ya ukweli, na 
kama kweli waraka huu umetoka makao makuu ya chama, sioni ni kwa nini 
jambo hili zito kiasi hiki haliletwi kwenye vikao vya chama na sisi 
tunaotuhumiwa kukivuruga chama tushughulikiwe kwa mujibu wa taratibu 
kama ambavyo watu wengi wamewahi kushughulikiwa ndani ya chama chetu kwa
 makosa waliyotenda. 
iv)
 Ni vizuri tukajenga utamaduni wa kuhoji mambo badala ya kuyameza kana 
kwamba tunasoma msaafu. Hivi huyo mtu anayemhonga Zitto bilioni mbili 
(2,000,000,000) ili atoe siri za chama, ni siri gani hizo ambacho chama 
cha siasa kinazo ambazo ni za hatari hata itolewe hongo kama hiyo? 
v)
 Ninasikitishwa na idara ya uenezi wa chama chetu kukaa kimya bila kutoa
 maelezo juu ya jambo hili, hasa pale ambapo tumeambiwa waraka huu 
umetoka makao makuu. Hii si kawaida kwa idara yetu hii nyeti 
iliyosheheni watu mahiri. Mara zote huwa wepesi kabisa kwa vijana wetu 
katika idara hii kutoa ufafanuzi, tena kwa mambo mepesi kabisa 
yanayokigusa chama, vipi makamanda kwenye jambo hili imekuwaje?
v)
 Mwisho kama kuna watu walidhani kwamba kwa uzushi huu watanikatisha 
tamaa na kunirudisha nyuma katika kutoa mchango wangu wa kuimarisha 
siasa ya vyama vingi hapa nchini, na kuijenga CHADEMA kama chama mbadala
 imara wamekosea. Nipo imara na nitaendelea kutoa mchango wangu 
kikamilifu. Poleni sana wote mliokwazwa na jambo na ufafanuzi wangu ndio
 huo.
 
 
 
          
      
 
  
  
 
0 Weka maoni yako hapa:
Post a Comment
COMMENT HAPA