Nov 11, 2013

Dr. Kitila Mkumbo( Mjumbe kamati kuu chadema) atoa Tamko


Kufuatia taarifa zinazosambazwa kwenye mitandao ya kijamii kuhusu kuhongwa kwa Zitto naye kuhonga watu wengine, nikiwemo mimi, ili kutoa siri za chama chetu (CHADEMA) kwa lengo ya kukivuraga watu, wengi sana wameniandikia email, sms na hapa fb ili nitoe ufafanuzi kuhusu ukweli wa mimi kuhongwa na Zitto na mahusiano yangu na mwanasiasa huyu nguli. Mwanzoni nilipuuzia na sikutaka kabisa nitoe maoni kuhusu jambo hili kutokana na kiwango cha ujinga kilichomo ndani ya waraka huo unaosambazwa. Hata hivyo kwa kuwa watu wengi wamenitaka nitoe ufafanuzi, napenda kueleza haya yafuatayo:

i) Mimi Kitila Mkumbo, pamoja na umaskini wangu, sijawahi kuhongwa popote na sitarajii kuhongwa. Taarifa zinazosambazwa juu yangu ni za uwongo wa kijinga na uzushi wa kitoto kwa malengo ya siasa nyepesi. Ni wazi kwamba wanaosambaza habari chafu juu yangu hawanijui na ndiyo maana wanaweza kudiriki kuzusha kwamba mie Kitila Mkumbo naweza kuhongwa sh. 200,000/=. Hakuna namna nyingine ya kuthibitisha kwamba waraka huu na maudhui yake ni mambo ya kutunga zaidi ya hilo la kuzusha kwamba nami ni miongoni mwa watu waliohongwa. 

ii) Kuhusu mahusiano yangu na Zitto ni kwamba kijana huyu ni rafiki yangu wa miaka mingi tuliyejuana na kuanza urafiki kabla ya hata mie kuijua CHADEMA. Urafiki wetu ulikuwepo, upo na utaendelea kuwepo ndani na/au nje ya siasa. Wasiopenda hili poleni sana. Mie ni mtu mzima na hakuna mtu yeyote mwenye uwezo wa kunichagulia marafiki na/au maadui. 

iii) Wanaosambaza waraka huu ni watu woga wa demokrasia na wasioijua CHADEMA. Chama hiki kimejipambanua kwa miaka mingi kwamba ni chama kinachopigania demokrasia ndani na nje ya chama. Matatizo yetu hushughulikiwa kikamilifu ndani ya vikao ambapo huwa tunajadili mambo kwa upana. Watu wenye makosa husutwa, huonywa na ikibidi huadhibiwa. Kama kweli haya yanayosambazwa yangekuwa na hata chembe ya ukweli, na kama kweli waraka huu umetoka makao makuu ya chama, sioni ni kwa nini jambo hili zito kiasi hiki haliletwi kwenye vikao vya chama na sisi tunaotuhumiwa kukivuruga chama tushughulikiwe kwa mujibu wa taratibu kama ambavyo watu wengi wamewahi kushughulikiwa ndani ya chama chetu kwa makosa waliyotenda. 

iv) Ni vizuri tukajenga utamaduni wa kuhoji mambo badala ya kuyameza kana kwamba tunasoma msaafu. Hivi huyo mtu anayemhonga Zitto bilioni mbili (2,000,000,000) ili atoe siri za chama, ni siri gani hizo ambacho chama cha siasa kinazo ambazo ni za hatari hata itolewe hongo kama hiyo? 

v) Ninasikitishwa na idara ya uenezi wa chama chetu kukaa kimya bila kutoa maelezo juu ya jambo hili, hasa pale ambapo tumeambiwa waraka huu umetoka makao makuu. Hii si kawaida kwa idara yetu hii nyeti iliyosheheni watu mahiri. Mara zote huwa wepesi kabisa kwa vijana wetu katika idara hii kutoa ufafanuzi, tena kwa mambo mepesi kabisa yanayokigusa chama, vipi makamanda kwenye jambo hili imekuwaje?

v) Mwisho kama kuna watu walidhani kwamba kwa uzushi huu watanikatisha tamaa na kunirudisha nyuma katika kutoa mchango wangu wa kuimarisha siasa ya vyama vingi hapa nchini, na kuijenga CHADEMA kama chama mbadala imara wamekosea. Nipo imara na nitaendelea kutoa mchango wangu kikamilifu. Poleni sana wote mliokwazwa na jambo na ufafanuzi wangu ndio huo.

0 Weka maoni yako hapa:

Post a Comment

COMMENT HAPA